Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Thursday 6 June 2013

Meghji alia riba benki zinaumiza wakopaji

                                   


 Waziri wa zamani wa Fedha, Zakhia Meghji, ameitaka Serikali kudhibiti benki ili ziache kuwatoza riba kubwa ya mikopo wananchi wa Tanzania.
Meghji, ambaye ni Mbunge wa Kuteuliwa, alisema riba ya kukopa iliyopangwa na Benki Kuu ni asilimia nane lakini benki hizo zimekuwa zikitoza riba ya asilimia 19.
Hata hivyo, gazeti hili linafahamu kiwango cha riba kinachotozwa na mikopo kwa sasa hufikia hadi asilimia 30 katika baadhi ya benki.
Akichangia hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Wizara ya Fedha kwa mwaka 2013/14 bungeni jana, Meghji alisema kwa mwenendo huo benki haziwezi kuwakomboa Watanzania kiuchumi. “Hata Gavana wa Benki Kuu anajua kuwa tunakopa fedha kwa benki kubwa kwa riba ya asilimia nane, lakini benki hizo zinakopesha kwa riba ya asilimia 19, hali hii inawapa shida wananchi na hasa wale wenye kipato cha chini,” alisema Meghji. Meghji, ambaye aliondolewa kwenye nafasi ya Waziri wa Fedha mwaka 2008, alilalamikia pia urasimu katika utoaji mikopo akitoa mfano baadhi ya benki kutaka makazi ya wakopaji huku wakisingizia wanataka vitambulisho vya taifa.
“Mfano hata sisi wabunge hapa tunashindwa kupata mikopo hiyo wakati tunajulikana tunaishi wapi, tunafanya nini na tunalipwa nini lakini bado ni matatizo, je hao wananchi inakuwaje?” alihoji. Naye Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila (NCCR-Mageuzi) alilia na benki akieleza kuwa haziwasadii Watanzania na akazituhumu kuwa zinajihusisha na kutorosha fedha nchini.
Kafulila alisema licha ya Tanzania kuwa na benki zaidi ya 50 lakini huduma za kibenki haziwafikii kikamilifu Watanzania walio wengi. “Hizi benki hazipo kwa ajili ya kumsaidia mwananchi….zipo kibiashara zaidi na ndiyo maana wanatoza riba kubwa hali inayomnyima mwananchi fursa ya kukua na badala yake wanaokopa wanazifanyia kazi benki,” alisema Kafulila. Pia aliitaka Serikali ipeleke bungeni majina ya watu wote waliokopa pesa katika Benki ya NBC ili wajulikane na walazimishwe kuzilipa.
“Zaidi ya shilingi 60 bilioni zimekopwa na wafanyabiashara wakubwa….wapo tu na hakuna mwenye nia ya kulipa, tunataka majina ya watu wote waliokopa katika benki hiyo yaletwe hapa bungeni,” alisema.
Ununuzi wa magari
Mapema akiwasilisha bungeni makadirio ya matumizi ya wizara yake, Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa alisema, Serikali itafuta ununuzi holela wa magari kwa taasisi zake mbalimbali, pia kupunguza muda kwa wastaafu kupata pensheni zao kutoka miezi sita hadi miezi mitatu.
Alisema taasisi zote za Serikali zitapaswa kununua magari kupitia Wakala wa Huduma ya Ununuzi Serikalini, (GPSA), kwa kuwa eneo la ununuzi wa magari linatumia fedha nyingi.
“Ununuzi wa magari ni eneo linalotumia fedha nyingi za umma na kutokana na hilo, Serikali imeona kuna umuhimu wa kuweka utaratibu bora utakaowezesha kupata thamani ya fedha katika ununuzi pamoja na matumizi ya magari yake.

0 comments:

Post a Comment