Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Thursday 4 July 2013

FBI waingia Arusha kuchunguza bomu la Soweto

                             

 Askari wa Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI), tayari wapo Arusha kushirikiana na polisi ili kuchunguza tukio la mlipuko wa bomu la kutupa kwa mkono kwenye mkutano wa kampeni za Chadema.
Katika tukio hilo lililotokea Juni 15, mwaka huu Viwanja vya Soweto, eneo la Kaloleni, Arusha, watu wanne walipoteza maisha huku zaidi ya 60 wakijeruhiwa.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Lebaratus Sabas, alithibitisha ushiriki wa FBI katika upelelezi huo.
Licha ya FBI, polisi wanashirikiana na wenzao kutoka nchi jirani ya Kenya, ambao wana uzoefu na matukio ya milipuko ya mabomu yanayotokea nchini mwao mara kwa mara, hasa baada ya nchi hiyo kupeleka wanajeshi nchini Somalia kukabiliana na Kundi la Al-Shabaab.
“Tunaendelea na uchunguzi wa kina mlipuko wa bomu Soweto, tayari wenzetu wa FBI na polisi wa Kenya wamefika kushirikiana nasi, nachukua fursa hii kuwaomba wenye ushahidi utakaosaidia upelelezi kujitokeza,” alisema Sabas.
Serikali imetangaza zawadi ya Sh100 milioni kwa yeyote atakayetoa taarifa itakayosaidia kumpata aliyehusika, au wanaohusika na mlipuko huo.
Sabas alisema watu watatu waliokuwa wakishikilia na polisi kwa mahojiano kuhusu bomu hilo, tayari wameachiwa kwa dhamana.
Hii ni mara ya pili maofisa wa FBI na polisi kutoka Kenya kushiriki uchunguzi wa mlipuko wa bomu Arusha.
Mara ya kwanza walishiriki kuchunguza mlipuko uliotokea kwenye Kanisa la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi, eneo la Olasiti iliyotokea Mei 5, mwaka huu.
Kwa mujibu wa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, bomu lililolipuka Soweto ni la kijeshi na limetengenezwa nchini China.
Uchaguzi wa madiwani kata nne za Elerai, Kimandolu, Themi na Kaloleni, uliahirishwa hadi Juni 30, mwaka huu kabla ya kusogezwa mbele tena hadi Julai 14, kwa kile kilichoelezwa na Mwenyekiti wa NEC, Jaji Damian Lubuva, kuwa sababu za usalama.
Wakati huohuo, Serikali imetangaza kugundua mtandao wa milipuko ya mabomu yaliyotokea Kanisa la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi, eneo la Olasiti na Viwanja vya Soweto, Arusha.

mwanzo Habari Kitaifa Kitaifa Mzee Mandela kuzikwa Qunu

                           

Gari la kubeba maiti likiwasili katika eneo la Mvezo Resort kuchukua mabaki ya miili ya watoto watatu wa Nelson Mandela iliyokuwa imezikwa kinyemela katika eneo hilo na mjukuu wa kiongozi huyo, Mandla. Picha na AFP.

 Vita ya wapi atakapozikwa  Rais wa kwanza mzalendo wa Afrika Kusini, Mzee Nelson Mandela imefikia tamati na sasa ni rasmi kwamba atazikwa Qunu uamuzi ambao umeacha ufa na uhasama mkubwa katika familia ya kiongozi huyo.
Jana, mabaki ya miili ya watoto watatu wa Mandela ambao ni marehemu ilitarajiwa kuzikwa upya katika eneo la Qunu, yakiwa ni mazishi ya mara ya tatu tangu walipofariki dunia katika vipindi tofauti, ukiwa ni utekelezaji wa amri ya Mahakama Kuu ya Eastern Cape.
Uamuzi huo ulimaanisha kushindwa kwa mjukuu wa Mandela, Mandla ambaye jana katika mkutano wake na waandishi wa habari alisema: “Sikusudii kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa Mahakama,” lakini akahusisha ugomvi katika familia ya babu yake kwamba ni vita ya fedha na mali za Mandela.
Mabaki hayo ni ya mtoto wa kwanza wa kiume wa kiongozi huyo, Makgato aliyefariki dunia 2005, binti yake wa kwanza Makaziwe (mkubwa) ambaye alifariki akiwa mchanga mwaka 1948 na mtoto wake wa pili wa kiume, Madiba Thembekile aliyefariki katika ajali ya gari 1969.
Mahakama Kuu ya Eastern Cape ilitoa uamuzi uliowapa ushindi wanafamilia 16 wa Mandela ambao walifungua madai wakiongozwa na shangazi yake Mandla, Makaziwe.
Jaji Lusindiso Pakade katika hukumu yake, mbali na kutoa amri hiyo alitaja vitendo vya Mandla kuwa ni vya aibu visivyo vya kibinadamu hivyo kutoa amri ya kufukuliwa miili hiyo na kisha kurejeshwa Qunu. Mabaki hayo yalihamishwa kutoka kijiji cha Mvezo ambako yalizikwa mara ya pili kwa kificho miaka miwili iliyopita na mjukuu mkubwa wa Mandela, Mandla ambaye pia ni kiongozi wa kimila katika kijiji hicho.
Kazi ya kufukua makaburi ya watoto wa Mandela katika eneo la Mvezo ilifanyika hadi juzi usiku chini ya ulinzi wa polisi baada ya madalali wa mahakama kutumia sururu kuvunja lango (geti) kuu la kuingia katika makazi ya Mandla.
Kwa mujibu wa msemaji wa polisi wa eneo hilo, Luteni Kanali Mzukisi Fatyela, uchimbuaji wa makaburi ulifanywa na wataalamu wa Kituo cha Afya cha Mthatha na baadaye kupelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha kituo hicho juzi usiku na jana asubuhi mabaki ya marehemu hao yalifanyiwa uchunguzi wa kimaabara kabla ya kupelekwa Qunu kwa maziko.

 
 

JICHO LETU MAGAZETINI LEO IJUMAA

                             

 













Jeshi la Misri latoa wito wa kudumishwa umoja

                               

Jeshi la Misri limetoa wito wa kudumishwa umoja baada ya kuondolewa madarakani serikali ya Muhammad Mursi na kuapishwa Adly Mansour kuwa rais wa mpito wa nchi hiyo. Taarifa iliyotolewa na jeshi imetaka kuimarishwa mshikamano wa kitaifa, haki na uvumilivu na kuongeza kuwa, hekima, utaifa wa kweli na kujenga maadili ya binadamu ni masuala yanayosisitizwa na dini zote na kwamba kuna haja ya kujiepusha na hatua za upande mmoja na za kiholela dhidi ya mrengo au kundi lolote la kisiasa. Jeshi la Misri aidha limesema, watu wanaweza kutumia haki yao madam hawavuki mipaka, kwani maandamano yasiyokuwa ya amani yanaweza kuhatarisha usalama na amani ya nchi.
Wakati huo huo harakati ya Ikhwanul Muslim ya Misri imeitisha maandamano ya kupinga hatua ya jeshi la nchi hiyo ya kumuuzulu rais Muhammad Mursi leo baada ya swala ya Ijumaa. Hayo yanajiri huku  duru za kiusalama zikiarifu kuwa, kiongozi mkuu wa harakati ya Ikhwanul Muslim ya Misri  Mohammed Badie amekamatwa na anashikiliwa mjini Cairo.  

 

Kenya yakanusha kuunga mkono machafuko Kismayo

                              

Wizara ya Ulinzi ya Kenya imekanusha tuhuma kwamba jeshi la nchi hiyo linachochea machafuko katika mji wa Kismayo, Kusini mwa Somalia. Taarifa ya wizara hiyo imesema jeshi la Kenya linafanya juu chini kuona amani na utulivu vinarejea Somalia. Serikali ya Somalia imelituhumu jeshi la Kenya kwamba limeshindwa kufanya kazi barabara na hivyo kusababisha mapigano ya hivi karibuni kati ya makundi tofauti yaliyosababisha vifo vya watu 65. Serikali ya Mogadishu imeuandikia barua Umoja wa Afrika ikisema Kenya imekuwa ikiegemea upande mmoja na kulipendelea kundi moja dhidi ya makundi mengine na ilimkamata afisa mmoja mkuu wa jeshi la Somalia akitumia silaha nzito katika maeneo ya raia katika eneo la Kismayo, kusini mwa Somalia. Kenya ina kikosi chake kusini mwa Somalia karibu na mpaka wake kama sehemu ya kikosi cha Umoja wa Afrika cha kulinda amani. Somalia imekuwa katika vita kwa miongo kadhaa sasa lakini matumaini yalikuwa kwamba kikosi cha Umoja wa Afrika wakiwemo wanajeshi wa Kenya wataleta tofauti kubwa katika nchi hiyo. Sasa Somalia inautaka Umoja wa Afrika kuchunguza madai hayo na iwapo yatabainika kuwa ya kweli basi jeshi la Kenya liondolewe nchini humo.
 

Mahakama kuu Zimbabwe kutoakhirisha uchaguzi

                       
Mahakama ya Katiba ya Zimbabwe imekataa ombi la serikali ya nchi hiyo la kubadilisha tarehe iliyoainishwa kwa ajili ya kufanyika uchaguzi wa rais na bunge. Serikali ya Harare ilikuwa imeitaka mahakama hiyo kuakhirisha tarehe ya uchaguzi.
Mei 31 Mahakama ya Katiba ya Zimbabwe ilitoa hukumu na kutangaza kwamba uchaguzi wa rais na bunge wa nchi hiyo unapaswa kufanyika kabla ya Julai 31 mwaka huu wa 2013. Suala hilo linapingwa na wapinzani wa Rais Robert Mugabe ambapo Waziri Mkuu wa Zimbabwe Morgan Tsvangirai anaona kuwa wanahitajia muda zaidi ili kutekelezwa marekebisho ya kimsingi nchini kabla ya uchaguzi. Uchaguzi wa Rais na Bunge jipya la Zimbabwe unatazamia kuhitimisha shughuli za serikali ya mseto na umoja wa kitaifa.

 

JICHO LETU MAGAZETNI LEO ALHAMIS