Jeshi la Misri limetoa wito wa kudumishwa umoja baada ya kuondolewa madarakani serikali ya Muhammad Mursi na kuapishwa Adly Mansour kuwa rais wa mpito wa nchi hiyo. Taarifa iliyotolewa na jeshi imetaka kuimarishwa mshikamano wa kitaifa, haki na uvumilivu na kuongeza kuwa, hekima, utaifa wa kweli na kujenga maadili ya binadamu ni masuala yanayosisitizwa na dini zote na kwamba kuna haja ya kujiepusha na hatua za upande mmoja na za kiholela dhidi ya mrengo au kundi lolote la kisiasa. Jeshi la Misri aidha limesema, watu wanaweza kutumia haki yao madam hawavuki mipaka, kwani maandamano yasiyokuwa ya amani yanaweza kuhatarisha usalama na amani ya nchi.
Wakati huo huo harakati ya Ikhwanul Muslim ya Misri imeitisha maandamano ya kupinga hatua ya jeshi la nchi hiyo ya kumuuzulu rais Muhammad Mursi leo baada ya swala ya Ijumaa. Hayo yanajiri huku duru za kiusalama zikiarifu kuwa, kiongozi mkuu wa harakati ya Ikhwanul Muslim ya Misri Mohammed Badie amekamatwa na anashikiliwa mjini Cairo.
0 comments:
Post a Comment