Mbunge wa kuteuliwa, James Mbatia ameitaka Serikali isiishie
kuivunja Kamati ya Ithibati ya Vifaa vya Elimu, (EMAC), na badala yake
iende mbali zaidi kwa kuwachukulia hatua za kisheria wajumbe wote wa
kamati hiyo.
Mbatia ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taifa wa
NCCR-Mageuzi alisema jana mjini Dodoma kuwa kamati hiyo inahusika moja
kwa moja kuua elimu nchini kutokana na kufumbia macho ufisadi ulioruhusu
kusambazwa kwa vitabu visivyo na ubora.
“Hawa ni wahujumu uchumi wa nchi yetu; wanahusika
kuididimiza elimu yetu... Inaonyesha wazi kuwa watunzi wa vitabu vile
hawakutumia mitalaa. Kutokuongozwa kwa mitalaa kumesababisha vitabu vile
kukosa ubora. Haiwezekani mwandishi, mhariri na mhakiki, awe mtu
mmoja.” alisema.
Mbatia alisema Emac imetoa ithibati kwa vitabu
vyenye maudhui yasiyo sahihi au dhaifu na ambayo hayamo kwenye
mihutasari huku baadhi yao vikiwa vimeiwakilisha vibaya Bendera ya Taifa
pamoja na Nembo ya Taifa kwenye baadhi ya vitabu hivyo.
Alisema miongoni mwa vitabu vilivyopitishwa na
Emac havina majina ya waandishi na kwamba badala ya jina la mwandishi
limewekwa jina la kampuni ya uchapishaji.
“Hakuna hata kitabu kimoja chenye wasifu wa
mwandishi na karibu vitabu vyote havina wahariri wakati ni lazima kila
kitabu kiwe na angalau mhariri mmoja” alisema Mbatia.
Alisema kasoro nyingine iliyopo katika vitabu
hivyo ni makosa mengi ya lugha iliyotumika kuandikia ambayo ni
Kiswahili, hali inayoonyesha kuwa vitabu hivyo havikupitishwa na Baraza
la Kiswahili la Taifa (Bakita).
“Aibu nyingine ipo katika maelezo ambapo eti
wameandika mitalaa ya shule za awali unamwezesha mwanafunzi kukua
kiuchumi, kisiasa na kijamii…na kwa wale wa shule ya msingi, wanasema
mtalaa unamsaidia mwanafunzi kupata uelewa wa lugha ya Kifaransa ili
aweze kupata ajira…Kweli mwanafunzi wa shule ya awali anatakiwa akue
kiuchumi, kisiasa na kijamii….na hii lugha ya Kifaransa inatoka wapi
katika mtalaa wa Tanzania” alihoji Mbatia.
Mbatia aliitaka Serikali vilevile iviondoe sokoni
vitabu vyovyote vya kiada na ziada vyenye maudhui potofu kama
inavyofanya kwa bidhaa nyingine zisizo na ubora.
“Adhabu zitolewe kwa watayarishaji na wamiliki wa
vitabu duni vitakavyoingizwa shuleni kinyume na taratibu ili kuzuia
matendo ya rushwa…chombo cha kupokea taarifa kutoka kwa wadau wa elimu
kuhusu vitabu duni kiundwe” alisema.
Alisema endapo Serikali itapuuza na kuviacha
vitabu hivyo visivyo na ubora kuendelea kutumika, ubora wa elimu utazidi
kuporomoka kwa sababu wanafunzi watalazimika kutumia vitabu visivyo na
ubora.
0 comments:
Post a Comment