Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe akitoa heshima za mwisho wakati wa
kuaga mwili wa Judith Moshi kwenye Kanisa la Kiinjili la Kilutheri
Tanzania (KKKT), Usharika wa Sokon One, Arusha jana. Picha na Filbert
Rweyemamu.
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na mbunge wa Arusha Mjini,
Godbless Lema jana, walijisalimisha Makao Makuu ya Polisi ya Mkoa wa
Arusha na kuhojiwa kwa zaidi ya saa nne kabla ya kuachiwa kwa
kujidhamini wenyewe huku wakitakiwa kurejea kituoni hapo, Julai 22,
mwaka huu.
Pia Mbowe na Lema wamemtaka Rais Jakaya Kikwete
kuunda tume huru ya uchunguzi wa kimahakama ili kuchunguza vurugu za
Arusha zilizoanza Jumamosi iliyopita baada ya bomu kurushwa kwenye
mkutano wa Chadema na kusababisha vifo pamoja na zile zilizofuatia
wakati polisi ilipowasambaratisha wafuasi wa chama hicho kwa mabomu
walipokusanyika kwenye Viwanja vya Soweto kwa lengo la kutoa heshima za
mwisho kwa marehemu.
Wakiongozwa na mawakili watatu, Mbowe na Lema waliwasili polisi saa 3.50 asubuhi na kuhojiwa hadi saa 9.10.
Viongozi hao walipokewa na Mkuu wa Upelelezi Mkoa
wa Arusha, Diwani Nyanda kabla ya kutenganishwa kwenye vyumba viwili
tofauti kwa mahojiano.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Mbowe, Lema na
wakili Albert Msando walitaja mambo mawili ambayo polisi waliwahoji
kwanza ikiwa ni ushiriki wao katika mkusanyiko usio halali kwenye
Viwanja vya Soweto, Jumanne iliyopita ambao ulisambaratishwa na polisi.
Jambo jingine ambalo polisi iliwahoji ni kauli yao
ya kuwa na ushahidi unaohusisha polisi na tukio la bomu lililorushwa
kwenye mkutano wa Chadema na kusababisha vifo vya watu wanne huku zaidi
ya 60 wakijeruhiwa.
Mbowe alisema kwa pamoja wamewaeleza polisi kuwa
hawaamini kama mkusanyiko wa Jumanne iliyopita haukuwa halali kwa sababu
waliruhusiwa kuzungumza na wananchi waliokusanyika ili kuwashawishi
watawanyike.
“Mkuu wa Polisi Wilaya (OCD) wa Arusha, Gilles
Mroto ndiye aliyeturuhusu kuzungumza na wananchi wale kuwataka
watawanyike na ndicho tulichofanya, lakini tukashangaa kuanza kupigwa
mabomu mara baada ya kuwataka watu wanaotaka kutoa heshima za mwisho kwa
marehemu kwenda Hospitali ya Mount Meru,” alisema Mbowe.
Alisema Mkuu wa Operesheni wa Polisi, Kamishna
Paul Chagonja kuwa naye aliyewaomba viongozi wa Chadema kuwatawanya
wafuasi wa chama hicho baada ya kuzuiwa kutoa heshima za mwisho katika
viwanja hivyo vinavyomilikiwa na Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha
(AICC).
Msimamo wa Mbowe
Kuhusu ushahidi anaodai unawahusisha polisi na
tukio la bomu, Mbowe alisisitiza kuwa Chadema kina ushahidi wa kutosha
kuthibitisha hilo lakini alisema hakitaukabidhi mikononi mwa polisi.
Alisema hakitafanya hivyo kwa kuwa jeshi hilo ni
watuhumiwa wakuu hivyo hawawezi kuwa na dhamira na nia njema katika
upelelezi wao. Alisema ndiyo maana badala polisi kuwaona ni msaada,
kimeanza kutoa vitisho kwa wote wanaosema waliwashuhudia askari
wakishambulia watu kwa risasi kabla ya kuondoka na aliyerusha bomu
kwenye gari lao.
0 comments:
Post a Comment