Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Tuesday 18 June 2013

‘Mabomu’ sasa yaanza kumlipukia Mzindakaya

                                    

Mbunge wa Sumbawanga Mjini, Hilary Aeshi, amemshukuru Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli kwa hatua yake ya kumpoka umiliki wa nyumba 16 za Serikali, Mbunge wa zamani wa Kwela, Dk Chrisant Mzindakaya.

Aeshi alimrushia lawama Mzindakaya kwa kujimilikisha na kupangisha nyumba 16 za Serikali kwa faida yake binafsi.
“Namshukuru sana Dk Magufuli kwani baada ya kumweleza jambo hili akasitisha mara moja mkatabahuu, sasa nyumba zimerudishwa mikononi mwa Serikali... Magufuli ni msikivu kwani ameshasitisha mkataba,” alisema Aeshi.
Mbunge huyo alipendekeza nyumba hizo zikarabatiwe na wapewe viongozi mbalimbali wa Serikali wakiwamo majaji, akitaka ziachwe nyumba mbili pekee kwa ajili ya kufikia viongozi wa kitaifa.
Mzindakaya maarufu Mzee wa mabomu, anadaiwa kupangisha nyumba ambazo zinamilikiwa na Wakala wa Nyumba Tanzania (TBA) mjini Sumbawanga.
Akichangia mjadala wa Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2013/14, Aeshi alisema Mzindakaya alipanga nyumba hizo kwa bei ya Sh50,000 kwa mwezi, naye akizipangisha kwa watu mbalimbali wakiwamo raia wa kigeni kwa dola 400 za Marekani kila mwezi kwa nyumba.
Alisema bei ambayo Mzindakaya alipangishwa nyumba hizo, hailingani bei ya soko eneo la Uzunguni mjini Sumbawanga.
“Zaidi ya miaka 15 Mzindakaya kapangishwa nyumba za Serikali, inakuaje nyumba hizo akapangishwa mtu mmoja halafu wakija wageni na viongozi wa Serikali anawapangisha, hivi Mzindakaya ni nani hasa?” alihoji Aeshi. Alisema Mzindakaya amekuwa akifanya kitendo hicho kinyume na mkataba wake wa upangaji, ambao unamzuia mpangaji wa nyumba kumpangisha mtu mwingine wa pili bila ridhaa ya mwenye nyumba.
Mbunge huyo alisema licha ya kupangisha nyumba hizo, Mzindakaya amekuwa akiibia Serikali kwa kukwepa kulipa kodi inayotokana na kupangisha nyumba hizo na kwamba, viongozi wanaohamia Mkoa wa Rukwa wamekuwa wakiishi hoteli kwa ukosefu wa nyumba.
“Mwenyekiti (Jenister Mhagama) napenda kumshukuru kwa dhati mheshimiwa Magufuli, kwa kuwa baada ya kupata taarifa hizi ameanza kuchukua hatua mara moja, ”alisema.

 

0 comments:

Post a Comment