Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Tuesday 14 May 2013

Wairani kumpigia rais kura katika nchi 120 duniani

                                 

Wairani wanaoishi katika nchi 120 kote duniani watakuwa na uwezo wa kupiga kura katika uchaguzi wa rais wa Iran utakaofanyika Juni 14.
Hayo yamedokezwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran anayeshughulikia Wairani waishio nje ya nchi Hassan Qashqavi. Amesema kuwa vituo zaidi ya 300 vya upigaji kura vitaanzishwa kote duniani kuwahudumia Wairani watakaopiga kura katika uchaguzi wa rais. Uandikishaji wa wagombea wa uchaguzi wa 11 wa Rais wa Iran ulimalizika Mei 11 huku watu 686 wakiwa wamejiandikisha. Kati ya vigogo mashuhuri waliojiandikisha ni rais wa zamani Ayatullah Hashemi Rafsanjani, Esfandyar Rahim-Mashaei ambaye ni mshauri wa karibu wa Rais Ahmadinejad, mwakilishi mkuu wa Iran katika mazungumzo ya nyuklia Saeed Jalili, meya wa Tehran Mohammad Baqer Qalibaf, waziri wa zamani wa mambo ya nje Ali-Akbar Velayati na msemaji wa wizara ya mambo ya nje aliyejiuzulu Ramin Mehmanparast. Majina ya watu waliojiandikisha yatawasilishwa kwa Baraza la Kulinda Katiba ambalo lina jukumu la kuchunguza na kuidhinisha watu waliotimiza masharti ya kugombea. Mshindi wa uchaguzi wa rais wa Juni 14 atachukua nafasi ya Rais Mahmoud Ahmadinejad anayemaliza muda wake na ambaye kwa mujibu wa katiba hawezi kugombea mara hii baada ya kuhudumu kwa mihula miwili mfululizo.
 

0 comments:

Post a Comment