Mtuhumiwa
mmoja kati ya tisa waliotiwa mbaroni kuhusiana mlipuko wa bomu katika
Kanisa la Joseph Mfanyakazi, Parokia ya Olasiti amefikishwa katika
Mahakama ya Hakimu Mkazi Wilaya ya Arusha na kusomewa mashtaka 21
yakiwamo ya mauaji na kujaribu kuua.
Mbele ya Hakimu Mkazi,
Devotha Kamuzora, mtuhumiwa huyo, Victor Ambrose (20), dereva wa
Bodaboda na mkazi wa eneo la Kwa Mromboo, Arusha alisomewa mashtaka hayo
yakiwamo matatu ya mauaji ya watu watatu waliofariki katika tukio hilo
lililotokea Mei 5, mwaka huu.
Wakisoma kwa kupokezana hati ya
mashtaka, Mawakili wa Serikali, Zachariah Elisaria na Haruna Matagane
walidai Calist pia anatuhumiwa kwa makosa 18 ya kujaribu kuua.
Mshtakiwa huyo alifikishwa mahakamani hapo kimyakimya akiwa chini ya
ulinzi wa maofisa wa polisi na hakutakiwa kujibu lolote kwa sababu
mashtaka yanayomkabili yanapaswa kusikilizwa na Mahakama Kuu.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Mei 27, mwaka huu itakapotajwa tena na mtuhumiwa amerudishwa mahabusu.
Saa moja kabla ya Ambroce kupandishwa kizimbani saa nne asubuhi,
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas aliitisha mkutano
na waandishi wa habari.
Waarabu (Waislamu) waachiwa huru
Polisi imewaachia huru raia wanne wa kigeni waliokuwa wakishikiliwa
kuhusiana na tukio hilo baada ya uchunguzi uliofanywa na Polisi wa
Tanzania, FBI na Polisi wa Kimataifa (Interpol) na kubaini hawakuhusika.
Kamanda Sabas aliwaambia waandishi wa habari ofisini kwake jana kuwa
raia hao walikamatwa baada ya kutiliwa shaka walipoonekana wakitoka
kwenye hoteli moja karibu na Kituo Kikuu cha Mabasi Arusha, muda mfupi
baada ya tukio hilo.
Raia watatu wa Falme za Kiarabu(UAE), walioshikiliwa na kuachiwa wamegundulika kuwa ni watumishi wa Serikali.
Kamanda Sabas aliwataja kuwa ni Abdul Azziz Mubarak (30), (Mamlaka ya
Mapato), Fouad Saleem Ahmed Al Hareez Al Mahri (29), (Zimamoto) na Daeed
Abdulla Saad (28), ambaye ni Askari wa Usalama Barabarani.
Raia hao pamoja na mwenzao, Al-Mahri Saeed Mohseen (29) kutoka Saudi
Arabia, walikabidhiwa kwa Idara ya Uhamiaji kuchunguzwa iwapo waliingia
nchini kihalali.
Pichani: Mtuhumiwa wa kurusha Bomu kwenye
Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph,Parokia ya Olasiti ,Jimbo Kuu la
Arusha,Victor Ambrose Calist akiwa kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi
Arusha baada ya kusomewa mashtaka 21 ya kuua na kujaribu kuua
0 comments:
Post a Comment