Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Sunday 5 May 2013

Rajoelina atangaza kuwa atagombea urais Madagascar


Rais Andry Rajoelina wa serikali ya mpito ya Madagascar amewashangaza wananchi wa nchi hiyo kwa kutangaza kuwa atagombea katika uchaguzi ujao wa rais.
Jina la Rais Andry Rajoelina aliye na umri wa miaka 38 limechapishwa katika faharasa ya jumla ya  majina 49 ya wagombea wa uchaguzi wa rais wa Madagascar uliopangwa kufanyika Julai 24 mwaka huu. Rajoelina alitwaa madarakani nchini Madagascar baada ya kuongoza mapinduzi mwezi Disemba mwaka 2009 yaliyomuengua madarakani Rais halali wa nchi hiyo  Marc Ravalomanana.
Baada ya miaka minne ya hali ya mgogoro na mivutano na kutokana na upatanishi wa viongozi wa Jumuiya ya Ustawi wa Kusini mwa Afrika (SADC) iliameliwa  kuwa uchaguzi mpya ufanyike huko Madagascar ili kutoa fursa ya kuchaguliwa serikali ya kidemokrasia. Huku akiwa chini ya mashinikizo ya kisiasa ya kieneo na kimataifa, Andry Rajoelina mwezi Januari mwaka huu alisisitiza kuwa hatagombea katika uchaguzi ujao wa rais wa Madagascar. 
Kwa mujibu wa mpango wa amani wa SADC, Rajoelina na Ravalomanana hawapasi kuwa wagombea katika uchaguzi huo. Kwa msingi huo hatua hiyo ya Rajoelina imewashangaza watu wengi. Akizungumza katika mahojiano na redio ya kimataifa ya Ufaransa, Andry Rajoelina amesema kuwa ameamua kuwa mgombea katika uchaguzi ujao wa rais wa Madagascar baada ya Lalao, mke wa Macr Ravalomanana rais aliyempinduwa na vilevile Didier Ratsiraka rais wa zamani wa nchi hiyo kutangaza kuwa wagombea katika uchaguzi huo.
Mapinduzi ya Madagascar ambayo yalilaaniwa na Umoja wa Afrika (AU) na Jumuiya ya Ustawi ya Kusini mwa Afrika (SADC) yameifanya nchi hiyo itengwe kieneo na kimataifa. Hii ni katika hali ambayo Rajoelina alipinga kurejea nchini rais aliyempindua lakini kwa mara kadhaa amemtaka Didier Ratsiraka rais wa zamani wa nchi hiyo arudi nchini humo. Ratsiraka ambaye aliiongoza Madagascar kwa muda wa miaka 23, naye pia ametangaza kuwa mgombea katika uchaguzi ujao wa rais nchini humo.
Madagascar ilikumbwa na mgogoro mwingine mwaka 2002 baada ya Ratsiraka kupinga ushindi wa Marc Ravalomanana, suala lililozusha mgawanyiko jeshini, bungeni na serikalini. Baada ya hapo Didier Ratsiraka alikimbilia nchini Ufaransa na hivi karibuni alirejea Antananarivo mji mkuu wa Madagascar baada ya kuishi Paris kwa muda mrefu na kutangaza rasmi kuwa mgombea wa kiti cha urais.

0 comments:

Post a Comment