Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Sunday 7 April 2013

Wanaotumia vibaya simu, mitandao ya kijamii kukiona

                     27Jumaadal ula,1434 Hijiriyah/ April 08,2013 Miyladiyah

SERIKALI imesema itachukua hatua kali za kisheria kwa atakayebainika kutumia vibaya simu za mkononi, na mitandao ya kijamii kuleta uchochezi au kwenda kinyume na maadili ya nchi.

Kauli hiyo ilitolewa jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki na Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Profesa Makame Mbarawa alipozungumza na waandishi wa habari na kusema kuwa lengo la kufanya hivyo ni kutaka kukomesha vitendo hivyo.

“Hatua hizo zitachukuliwa dhidi ya kampuni au mtu yeyote atakayetoa kashfa na kuitukana serikali, viongozi wa serikali, dini, siasa na watu binafsi,” alisema na kuongeza kuwa vitendo hivyo vinakiuka sheria za nchi.

Alisema hatua hizo pia zitawakumba watu wote wanaojihusisha na uonyeshaji wa picha za ngono kwenye mitandao, unyanyasaji wa watoto na ukiukaji wa maadili na kutoa taarifa zenye lengo la kuvunja utulivu na amani.

“Matumizi mabaya ya teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA) kama simu za mikononi, barua pepe, na mitandao ya kijamii yanafanywa na watu wachache kwa kusambaza taarifa zenye nia ya kuchafua taifa letu,” alisema.

Alisema pamoja na kwamba teknolojia hiyo katika miaka ya karibuni imechangia kuleta maendeleo makubwa nchini, baadhi ya watu wanaitumia kwa mambo yasiyofaa.

Aliendelea kusema kuwa watu wengine wamekuwa wakiitumia kwa kufanya wizi, ujambazi, ubakaji, biashara ya dawa za kulevya na ukahaba na kusambaza siri za watu binafsi bila idhini ya wahusika.

Aidha, alisema pia hatua kali zitachukuliwa kwa wakala au kampuni ya simu yoyote itakayouza SIM card kwa mtu yeyote bila ya kuwa na kitambulisho kinachotambulika kisheria.

Alisema pia ni kosa la jinai kutoa taarifa za uongo wakati wa usajili wa SIM card  na serikali imejipanga kuzima zote ambazo hazijasajiliwa.

0 comments:

Post a Comment