Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Saturday 8 June 2013

Rasimu ya Katiba chungu kwa CCM

                               

Mwanzoni mwa wiki hii Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilizindua rasimu ya Katiba Mpya iliyopendekeza kuwapo kwa mabadiliko makubwa kwenye mfumo wa utawala nchini, huku yakionekana kuwa machungu kwa chama tawala cha CCM.
Tayari CCM kimetangaza kufanya mkutano wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama hicho ili kuichambua na kujadili kwa kina rasimu hiyo ya Katiba Mpya.
Jana vyombo vya habari vilimnukuu Katibu Mkuu wa chama hicho Abdulrahman Kinana katika mkutano wake na waandishi wa habari akisema kuwa wataichambua na kuijadili rasimu hiyo.
Pamoja na mambo mengine, rasimu hiyo ya Katiba Mpya imependekeza kuwapo kwa Serikali tatu; Shirikisho la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali ya Tanzania Bara na Serikali ya Zanzibar, kuruhusiwa kwa mgombea binafsi na kufutwa kwa viti maalumu vya ubunge.
Mapendekeo hayo yametolewa ikiwa ni miezi sita tangu vyama mbalimbali vya siasa kuwasilisha maoni yao kwa tume hiyo inayoongozwa na Jaji Joseph Warioba na kupendekeza mambo mbalimbali ikiwamo muundo wa Serikali, Uchaguzi Mkuu na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).
Mapendekezo ya CCM
Katika mapendekezo yake CCM walitaka ubaki mfumo wa Serikali mbili kama ilivyo sasa, ikieleza kuwa hauna gharama, huku kikieleza kwamba uzoefu katika nchi nyingi za Afrika unathibitisha kushindwa kwa mfumo wa Serikali tatu na ule wa Serikali ya Shirikisho (Federation government).
Hata hivyo, mapendekezo ya rasimu hiyo yanaonyesha kuwa Jamhuri ya Muungano itakuwa na muundo wa shirikisho lenye Serikali tatu na kwamba shughuli zote za muungano zitasimamiwa na Serikali, Bunge na Mahakama ya Jamhuri ya Muungano, hivyo kukifanya CCM kuanguka katika maoni kuhusu suala hilo.
CCM ilipendekeza sera ya dola kutokuwa na dini rasmi, bali iruhusu kila mtu kuwa na uhuru wa kufuata dini anayoitaka mwenyewe, jambo ambalo limebaki kama lilivyo katika mapendekezo ya rasimu hiyo.
Chama hicho kimeonekana kukwama pia katika mapendekezo yake ya kuupigia debe mfumo wa sasa wa rais kushinda kwa wingi wa kura (simple majority) kwa maelezo kuwa hauna gharama pamoja na kutaka wananchi wawe na haki ya kuhoji uchaguzi wa rais.
Lakini, mapendekezo katika rasimu hiyo yanaeleza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano atatangazwa baada ya kupata zaidi ya asilimia 50 ya kura zote na endapo hakutakuwa na mshindi, walioshika nafasi ya kwanza na ya pili watarudia uchaguzi ndani ya siku 60.
CCM kilipendekeza mawaziri wasitoke nje ya Bunge, huku kikitaka kuongezwa kwa wigo wa viongozi wanaoteuliwa na rais na kupitishwa na Bunge kama ilivyo kwa waziri mkuu.
 

0 comments:

Post a Comment