Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo,
amesisitiza kuwa mpango wa kuchimba madini ya urani bado uko palepale na
kwamba hiyo inatokana na Serikali kujiridhisha na hatua zote.
Profesa Muhongo aliyasema hayo jana jijini Dar es
Salaam alipokuwa akizungumza na watalaamu kutoka Umoja wa Ulaya (EU),
kuhusu namna ya kutekeleza uchimbaji huo unaotarajiwa kuanza hivi
karibuni.
Alisema mpango huo utatekelezwa baada ya kukamilika kwa taratibu zote muhimu.
Waziri huyo alisema Serikali imejiridhisha kwamba
madini hayo hayatakuwa na madhara na kwamba tahadhari zote muhimu
zimeshachukuliwa.
Alisema hatua hizo zimefanywa huku kukiwa na upotoshaji unaoenezwa na baadhi ya watu wasiopenda maendeleo ya nchi.
“Madini hayo yatachimbwa kama tulivyopanga na
hatua zote stahiki zimeshachukuliwa kuhusu jambo hilo. Nawaomba wananchi
wasiwe na wasiwasi juu ya mpango huu,” alisema Profesa Muhongo.
Aliwataka wananchi wapuuzie upotoshaji unaoenezwa
dhidi ya mpango wa kuchimba madini hayo utakaofanywa na Kampuni ya
Mantara, kuwa utakuwa na madhara kwa binadamu.
Kwa upande wake, Balozi wa EU nchini, Fillberto
Sebregond alisema wamejipanga ipasavyo kuhakikisha kuwa uchimbaji huo
unakwenda vizuri na bila madhara kwa binadamu.
Alisema lengo ni kuhakikisha kuwa Tanzania inapata mapato yatakayotokana na uuzaji wa madini hayo.
“Tuna ushirikiano mzuri na nchi hii na tutasaidia
maeneo yote yatakayochimbwa madini hayo ili kuhakikisha kuwa wananchi
wanaishi katika hali ya usalama na bila madhara yoyote,” alisema Balozi
Sebregond .
Mkurugenzi wa Kampuni ya Mantara, Asa Mwaipopo
alisema kazi ya kuchimba madini hayo katika eneo la Mkuyu wilayani
Namtumbo, inatarajia kuanza hivi karibuni.
Alisema kazi hiyo imepangwa kuanza katika kipindi
hiki cha kiangazi kwa sababu wakati wa masika maeneo hayo yanakuwa na
matatizo.
0 comments:
Post a Comment