Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Saturday 15 June 2013

Bajeti vilio kila kona, wananchi waikosoa

                        
Watu wengi walikosoa upandishaji wa kodi na ushuru wa bidhaa na huduma kwamba utawadidimiza walalahoi.
Bajeti ya 2013/14 iliyotangazwa bungeni juzi na Serikali, imesababisha malalamiko na manung’uniko kutoka kila upande wa nchi, huku baadhi ya wasomi, wanasiasa na wananchi wakiiponda kwamba haiwezi kubadili hali ya maisha ya watu wa chini.
Wengi wanakosoa nyongeza ya kodi na ushuru mbalimbali ambazo wanasema zinazidi kudhoofisha hali ya watu wa chini, kwani gharama za maisha zitazidi kupanda na kwamba hali hiyo inawaneemesha walionacho.
Katika maoni yao kuhusu bajeti hiyo iliyosomwa na Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa, wapo waliokosoa vikali misamaha ya kodi ambayo wameitaja kwamba inadhoofisha uchumi wa nchi.
Mhadhiri wa Uchumi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Humphrey Moshi aliuambia mkutano wa wadau wa uchumi ulioandaliwa na Kampuni ya Ukaguzi wa Hesabu (KPMG) jana jijini Dar es Salaam kwamba, Serikali imeshindwa kukusanya kodi kwa wawekezaji wakubwa.
“Misamaha ya kodi inatolewa kwa wawekezaji wakubwa na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) inasababisha mzigo kwa Serikali. Hizi kampuni kama za simu na madini zinapokuja kuwekeza zinatafuta faida, hakuna sababu ya kuzisamehe kodi,” alisema Profesa Moshi.
Mchumi huyo alikosoa upandishaji wa kodi kwenye mafuta akisema kuwa itapandisha mfumuko wa bei kwa wananchi wa chini. “Huwezi kupandisha kodi ya mafuta, kwani ni chanzo cha kukua kwa mfumuko wa bei kwa kaya. Nilishafanya utafiti katika hilo… ni kweli mfumuko umeshuka, lakini kwa ngazi ya kaya bado bei ya bidhaa haijashuka. Tuna bahati tu mvua imenyesha mwaka huu,” alisema.
Hata hivyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Tafiti kuhusu Kuondoa Umaskini (Repoa), Profesa Samuel Wangwe alisema ni bajeti nzuri ambayo inalenga kuchochea maendeleo. Alisema ili kuhakikisha mapato mengi yanakusanywa ni lazima kuendana na ukuaji wa teknolojia yenye lengo la kuwabaini wanaokwepa kodi. “Wale ambao hawataki kulipa kodi kwa kutumia mifumo mipya, TRA itawabaini na kuongeza mapato ya taifa,” alisema Profesa Wangwe.
Wasomi wengine
Kwa upande wake, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Dk Prosper Ngowi alisema Serikali imeendeleza utaratibu aliouita kuwa ni mbovu wa kutegemea kukusanya kodi kutoka vyanzo vya anasa.
“Unapoweka kodi katika sigara, vinywaji na kutuma fedha kwa njia ya simu bado si sahihi, kwani vitu hivi vinawahusu watu wa hali ya chini hivyo unaendelea kuwaumiza wananchi wenye hali ngumu ya maisha,” alisema Dk Ngowi.
Naye Mwenyekiti wa Infotech Investment Group, Ali Mufuruki alisema suala la matumizi linatakiwa kuangaliwa upya kwa sababu hakuna tofauti ikilinganishwa na miaka ya nyuma.
 

0 comments:

Post a Comment