Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Saturday 15 June 2013

Misamaha ya kodi kwa mboga yapoteza Sh503bilioni

Wakati wananchi wakilalamikia ongezeko la tozo za ushuru na kodi mbalimbali katika bajeti ya Serikali ya 2013/14, imebainika kuwapo misamaha ya ongezeko la thamani (VAT) kwa bidhaa mbichi za kilimo, mifugo na mazao hupoteza mabilioni ya shilingi kila mwaka.
Uchunguzi unaoonyesha kuwa misamaha hiyo imekuwa ikitolewa kwa miaka sita mfululizo na kuligharimu taifa wastani wa Sh503bilioni, fedha ambazo zingetosha kwa bajeti ya wizara kumi za Serikali kwa mwaka wa fedha 2013/2014
Bidhaa na vitu ambavyo vimekuwa vikipewa misamaha hiyo ni pamoja mazao ya kilimo vikiwamo nafaka na mbogamboga pia wanyama na ndege wa kufugwa na vitu hivyo vinapatikana kwa wingi hapa nchini.
Licha ya misamaha ya kodi kuwepo kisheria, lakini imekuwa ikitumika vibaya, hata mazao ya kilimo na mifugo inayopatikana kwa wingi pia nchini. Mazao haya yamekuwa yakisamehewa kodi hiyo, hivyo kuathiri uzalishaji wa ndani.
Mmoja wa watumishi katika Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) aliliambia gazeti hili kuwa: “Hakuna uchambuzi wa bidhaa hizo, wala kuzichuja; ni holela hasa maana ya kuwa holela. Utaratibu huu ni mbaya wala hautufai kwa namna yeyote ile”.
Bajeti yake kuu ya Serikali kwa mwaka ujao wa fedha iliyotangazwa juzi inaonyesha kusheheni kwa ongezeko la kodi na ushuru katika baadhi ya bidhaa, zikiwamo mafuta, soda, vinywaji vikali, simu na matumizi yake pamoja na leseni za magari, hatua inayolenga kupata fedha za kugharimia shughuli zake mbalimbali.
Hata hivyo takwimu zilizopatikana kutoka ndani ya TRA zinaonyesha kuwa kwa miaka sita; kati ya 2003 na 2008, Serikali imesamehe kodi katika bidhaa hizo ikiwamo mboga, ambayo kama ingetozwa kwa bidhaa hizo ingeliingizia taifa zaidi ya Sh503 bilioni.
Kiasi hicho cha fedha ni kikubwa kikilinganishwa na bajeti ya jumla ya Sh497.346 bilioni iliyopitishwa na Bunge kwa ajili ya matumizi ya wizara kumi za Serikali kwa mwaka ujao wa fedha (2013/14).
Wizara hizo na fedha zilizotengewa kwenye mabano ni Ofisi ya Makamu wa Rais - Muungano na Mazingira (Sh55,682,428,000), Wizara ya Maliasili na Utalii (Sh75,681,745,000), Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo (Sh30,328,045,000), Ushirikiano wa Afrika Mashariki (Sh20,470,107,000) na Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi (Sh67,180,225,000).
Wizara nyingine ni Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia (Sh63,147,599,460), Ofisi ya Rais – Mipango (Sh 37,696,984,000), Kazi na Ajira (Sh14,958,896,000), Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto (23,870,448,700) na Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi (Sh108,330,273,040).
Tangu Jumatano wiki hii gazeti hili lilizungumza na Mkurugenzi wa Idara ya Elimu na Huduma kwa Walipa Kodi wa TRA, Richard Kayombo ofisini kwake jijini Dar es Salaam, kuhusu misamaha hiyo, lakini hadi jana jioni aliomba apewe muda zaidi kwa kile alichosema kuwa ni kufanya ulinganisho wa takwimu.

0 comments:

Post a Comment