Kamati iliyoundwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk
Emmanuel Nchimbi kuchunguza madai ya Polisi kufanya vurugu wakati wa
kutuliza ghasia zilizozuka Mjini Mtwara wiki iliyopita, leo inaanza kazi
ya kutathmini athari zilizojitokeza.
Kazi hiyo itafanywa kwa kushirikiana na Kamati ya
Maafa ya Wilaya Mtwara na Mkuu wa Wilaya hiyo, Wilman Ndile alisema jana
kuwa wananchi wote waliopatwa na maafa, wanatakiwa kufika katika ofisi
yake kufanyiwa tathmini ya mali zao zilizoharibika na athari nyingine
zilizotokana na vurugu hizo.
“Tumewapa maelekezo wananchi waliopata maafa
wafike Ofisi ya Wilaya kwani hata Tume ya Waziri wa Mambo ya Ndani
kuzungumzia uovu wa maaskari itakuwapo kusikiliza. Wengi wanailalamikia
Polisi kujihusisha na hujuma. Tunawataka wananchi kuja na vielelezo
zikiwamo picha,” alisema.
Juu ya kwamba Serikali itafidia hasara
iliyopatikana, Ndile alisema hakuna mpango huo lakini Kamati ya Maafa
itakaa kuangalia nini cha kufanya kwa wananchi hao.
Wananchi wengi walioathiriwa na vurugu hizo wanatoka katika maeneo ya Mikindani, Magomeni, Chikongola, Ufukoni na Mitengo.
Mbunge afanya ziara
Baada ya juzi kukataa kuongozana na Waziri Mkuu,
Mizengo Pinda kwa madai kuwa ziara yake haikuhusisha kuwatembelea
wananchi walioathirika katika vurugu hizo, jana Mbunge wa Mtwara Mjini
(CCM), Hasnein Murji alitembelea maeneo yaliyoathirika kuwapa pole
wakazi wake na kuwataka wawe na amani, kufanya kazi zao kama kawaida
bila kuingia kwenye misigano na Serikali.
“Si sawasawa kushindana na Serikali. Kila mtu afanye kile kinachomhusu,” alisema akiwa Mikindani.
Mbunge huyo alimpatia Sh50,000 mwanafunzi wa
darasa la pili katika Shule ya Msingi Naida, Mikindani, Baraka Juma (11)
kwa ajili ya kununulia sare za shule na madaftari ambavyo vyote
viliteketea baada ya nyumba yao kuchomwa moto.
Mbunge huyo aliwataka wazazi kuwausia vijana wao
kutojihusisha na makundi ya vurugu kwani kufanya hivyo kunahatarisha
maisha yao.
Diwani wa Kata ya Magengeni, Omary Nawatuwangu
alisema nyumba zilizochomwa kwenye kata yake ni tano na tatu zilivunjwa
pamoja na vibanda vinane vya biashara.
0 comments:
Post a Comment