Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Tuesday 16 April 2013

Uhuru afungua rasmi bunge la Kenya

Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya leo amefungua rasmi Bunge la 11 la nchi hiyo na kubainisha sera muhimu za serikali yake. Katika hotuba yake mbele ya kikao cha pamoja cha Bunge na Senate mjini Nairobi, Rais Kenyatta amesema ataunda baraza dogo la mawaziri na kuimarisha utendaji wa mashirika ya kiserikali. Amesema atachukua hatua za haraka kumaliza ufisadi uliokita mizizi serikalini. Aidha Rais Kenyatta amebainisha ajenda ya kitaifa yenye nguzo tisa kama vile uwazi katika huduma kwa umma, kubuni nafasi za ajira, elimu, usalama, miundombinu bora na serikali ya ugatuzi. Aidha amesema, serikali yake itahimiza ustawi wa viwanda na kilimo. Kwingineko Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amesema, uchaguzi uliofanyika hivi karibuni unaonesha kuwa, Kenya ni mfano mzuri wa kuigwa hasa kuhusu namna ambavyo mzozo wa baada ya uchaguzi unaweza kutatuliwa kwa njia za amani. Ban ameyasema hayo alipohutubia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa jana Jumatatu kuhusu namna ya kutabiri, kuzuia na kukabiliana na mizozo Afrika. Akizungumza katika kikao hicho Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda Louise Mushikiwabo ameikosoa vikali Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC na kusema inatumiwa kisiasa. ICC inalaumiwa na viongozi wa Afrika kuwa ina malengo ya kisiasa na kibeberu katika kufuatilia madai yake dhidi ya Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya na naibu wake, William Ruto.

0 comments:

Post a Comment