Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Wednesday 24 April 2013

Sababu za walimu kukacha vituo vya kazi zaelezwa



Uongozi wa Mtandao wa Elimu Tanzania (TAN/Met) umetaja sababu mbalimbali zinazowafanya baadhi ya walimu kuacha kazi pamoja na kutoripoti kwenye vituo wanavyopangiwa.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mtandao huo, Mary Soko, alisema hayo jana alipokuwa akitoa salam kwenye Maadhimisho ya Wiki ya Uhamasishaji Elimu Duniani, ambayo kitaifa yanafanyika kwa juma moja mkoani Lindi.

Akiwasilisha salamu za mtandao huo, Soko alisema baadhi ya walimu wanalazimika kuacha kazi na kutafuta ajira zingine kutokana changamoto mbalimbali zinazowakabili, ikiwemo maslahi duni na mazingira duni, na kutothaminiwa kwa kazi wanazozifanya.

Alitaja sababu nyingine kuwa ni, kutopatiwa motisha na vifaa na zana muhimu za kufundishia na kujifunzia na  kukosekana kwa mazingira mazuri ya kuishi.

Aliwasisitiza Watanzania wakiwemo wa mkoa wa Lindi kuendeleza mijadala na makongamano kuhusu elimu ili kubaini matatizo yanayoikabili sekta hiyo hapa nchini.

Akizindua maadhimisho hayo kwa niaba ya Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk, Shukuru Kawambwa, Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Dk. Nassoro Hamidi, alisema kwa mwaka 2012 na 2013 serikali imeajiri walimu 26,460, kati yao 13,527 ni wa shule za awali na msingi, wakati 12,933 ni wa shule za sekondari.

Hata hivyo, alisema kati ya walimu 743 waliopangwa mkoani Lindi katika kipindi cha mwaka 2012 na 2013 walioripoti kwenye vituo vyao vya kazi ni 509 tu, huku 234 wakiwa hawajulikani walipo.

0 comments:

Post a Comment