Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Sunday, 13 January 2013

TAMKO LA WANACHUO, WAFANYABIASHARA NA WAKAZI WA IRINGA WANAOTOKA MIKOA YA LINDI NA MTWARA  KUPINGA USAFIRISHAJI WA GESI ASILIA TOKA MNAZI BAY- MTWARA KWENDA DAR ES SALAAM.
Ndugu, Waandishi wa Habari na Wananchi wote mliohudhuria hapa kufuatia maandamano ya wakazi wa Mkoa wa Mtwara yaliyofanyika mnamo tarehe  13 Januari 2013 sisi kama Wanavyuo,Wafanyabiashara na Wakazi wa Iringa tunaotoka mikoa ya Lindi na Mtwara na wadau wengine tunaungana na wenzetu wa Lindi na Mtwara KUPINGA VIKALI USAFIRISHAJI WA GESI ASILIA toka Mnazi Bay - Mtwara kwenda Dar es Salaam. Tumeamua kufanya hivi kutokana na sababu za msingi zenye maslahi kwa maendeleo ya Taifa zima la Tanzania sio tu Mikoa ya Lindi na Mtwara kama inavyodaiwa na baadhi ya viongozi mbalimbali wa serikali na vyama vya siasa. Zifuatazo ni sababu zinazotufanya tupinge usafirishaji wa gesi asilia toka Mtwara kwenda Dar es Salaam;
1.   Sisi kama wazawa,wakazi wa mikoa ya Kusini mwa Tanzania tuna haki ya kupigania haki  kutokana na dhulma  yeyote itakayofanyika kwa Watanzania wowote wale na popote pale ndani na nje ya nchi hii.
2.   Kisheria na katika  hali ya kawaida rasilimali yoyote ile inayopatikana katika eneo fulani ni lazima iwanufaishe wananchi waiishio katika eneo husika, hivyo rasilimali iliyopo mikoa ya Lindi na Mtwara ni lazima wananchi wanufaike,  kwani waswahili husema “Jungu kuu halikosi ukoko” na “Mgeni aje mwenyeji apone” hivyo kusafirishwa kwa gesi kutawadhoofisha wakazi wa Lindi na Mtwara na kujihisi kuwa pengine wao si wazawa wa Taifa hili.
3.   Pia kumekuwa na dhulma nyingi za rasilimali na kuzorotesha miradi mbalimbali ya maendeleo katika mikoani Lindi na Mtwara. Kwa mfano;
a)   Kuondolewa kwa Mashine ya kuvuta maji katika vijiji vya Namitema na Chihanga wilayani Newala kwa madai kuwa ni mbovu hatimaye kupelekwa kutumika mkoani Dodoma.
b)  Pia kuondolewa kwa taa zenye mwanga mkali katika uwanja wa ndege wa Mtwara na kupelekwa katika viwanja vingine mkoani Arusha.
c)    Ubabaishaji uliofanywa na serikali juu ya ahadi ya kukarabati Bandari ya Mtwara, bandari yenye kina kirefu Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika na hatimaye kujenga bandari mpya kwa kuchimba chini ya bahari ili kupata kina kirefu huko Bagamoyo.
d)  Kuahirisha ujenzi wa kiwanda cha Samaki Mkoani Mtwara na hatimaye kwenda kujengwa Dar es Salaam.
e)   Ubabaishaji wa bei za korosho kupitia utaratibu mbovu wa stakabadhi ghalani bila kuwashirikisha wakulima wa korosho. Utaratibu  ambao kwa asilimia kubwa unawanyonya wakulima wa zao la korosho ambalo ndio zao kuu la biashara mkoani humo. Kwa mfano;kulipwa kwa mkopo 70% awamu ya kwanza na 30% ni awamu ya pili na wakulima wengine hawalipwi kabisa.
f)    Kuwazuia wakulima kulima baadhi ya mazao mengine ya biashara mfano; Pamba kwa madai kwamba mazao hayo yataharibiwa na wadudu toka nchi jirani ya Msumbuji, madai ambayo hayana ukweli  wowote ule kwani hakuna utafiti wa kisayansi uliofanyika.
g)   Kutokamilika kwa barabara km. 60 toka Muhoro mpaka Somanga ikiwa sasa yapata miaka takribani 10, barabara muhimu sana ambayo inaunganisha mikoa ya ukanda wa kusini mwa Tanzania yaani Lindi na Mtwara wakati maeneo mengine katka nchi hii km. 300 hukamilika kwa muda mfupi tu.
h)  Kuzorota kwa elimu katika mikoa ya Lindi na Mtwara takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kuwa matokeo ya Kidato cha pili 2012 Mikoa ya Lindi na Mtwara  imeshika mkia Kitaifa haina maana kwamba ndugu zetu hawana akili ndio maana sisi wengi wetu tuko Vyuo Vikuu, isipokuwa serikali  ina usimamamizi mbovu kama vile Upungufu wa waalimu nk.
4.   Kusafirisha gesi kupeleka Dar es Salaam ni kuendeleza tatizo la ongezeko la idadi ya watu jijini Dar es Saalam kama vile wamachinga ambao asilimia kubwa wanatoka mikoa ya kusini yaani Lindi na Mtwara kuja kufanya biashara ndogondogo jijini Dar es Salaam.
5.   Kadhalika tunawalaani  viongozi wa serikali ambao wanahujumu maendeleo ya kusini wengine ni wakazi wa Mikoa ya Kusini wameonyesha usaliti wa wazi kabisa kwa wananchi wao wanaowawakilisha, hivyo basi tunawapa taarifa kuwa hatuna imani nao tena ya kutuwakilisha wananchi wa Lindi na Mtwara.
6.    Tumekerwa na baadhi ya kauli za viongozi wa Serikali na Vyama vya Siasa juu ya wakazi wa Mtwara kuhusu gesi.Mfano.Ndugu,Mwigulu Nchemba ambaye ni Naibu Katibu wa CCM Taifa alitoa kauli chafu   katika mkutano wa CCM Taifa Kibaha tarehe 30 Desemba 2012.
7.   Mikoa ya kusini haina vitega uchumi vikubwa vya kuliingizia pato taifa pamoja na wananchi wa kusini, hivyo hii ni fursa pekee kwa serikali kuleta chachu ya maendeleo kwa wakazi hawa wa kusini na sio kuwatelekeza kwa kusafirisha gesi kwenda Dar es Salaam.
8.   Tunalaani jeshi la polisi kwa kuwachukulia hatua wale wanaofanya mikutano ya kuhamasisha wananchi kupinga kauli ya serikali ya kusafirisha gesi kwenda Dar es Salaam.
9.   Katika mikoa ya Lindi na Mtwara toka uhuru kuna kero kubwa ya umeme, sasa hii ni fursa pekee kwa wakazi hawa wa kusini kuondokana na kero hii ya giza totoro. Kwa mfano; Wilaya ya Nanyumbu hakuna umeme kabisa  na wilaya zingine umeme usio na uhakika kama vile Masasi,Nachingwea,Liwale, Tandahimba, Newala na Ruangwa.      
Kufauatana na hali hiyo sisi tunaitaka serikali izingatie yafuatayo kuhusu gesi asilia iliyogundulika Mkoani Lindi na Mtwara;
1.   Kwa kuipunguzia serikali gharama katika mchakato wa ujenzi wa mabomba ya kusafirisha gesi umbali  wa km.560 toka Mtwara hadi Dar es Salaam kutumia Tsh.trilioni 1.9 iliyokopwa,  badala yake ijenge kiwanda cha gesi hiyo katika mikoa ambako rasilimali hiyo inapatikana.
2.    Kutakana na umuhimu mkubwa wa gesi hii kwa uchumi wa taifa basi kuwe na muda wa kutosha kwa wananchi kufanya mjadala juu ya  gesi kwani hadi sasa kuna mvutano kati ya serikali na wananchi na hii ndio demokrasia ya kweli.
3.   Kulipa nafasi Bunge tukufu kuangalia upya sera na sharia za gesi pamoja na madini mengine kama vile Uranium.
4.   Serikali iheshimu na kuthamini mawazo na matakwa ya wananchi na sio kufanya maamuzi kibabe kwani kufanya hivyo ni kukiuka kanuni na taratibu za utawala bora na demokrasia ya kweli.
5.   Tunamkumbusha Mh. Rais Jakaya Mrisho Kikwete ahadi yake ya mwaka 2009-2010 iliyopo katika ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) aliahidi kwamba mikoa ya Kusini (Lindi na Mtwara) itakuwa ni Ukanda wa Viwanda na akawahimiza wakazi wa Mtwara kujenga hoteli za kisasa za kutosha, zimejengwa lakini wanalala wenyewe tu, sasa ikiwa gesi asilia itasafirishwa kupelekwa Dar es Salaam ni viwanda gani tena ambavyo vitajengwa? Hii inaonyesha dhahiri kuwa serikali inataka kuitelekeza mikoa ya kusini katika taswira ya maendeleo ya taifa la Tanzania.
6.   Rais asiwaone viongozi wa siasa kama wachochezi kwa serikali na wanajitafutia umaarufu bali wanaungana na wananchi wa Lindi na Mtwara kupinga usafirishaji wa gesi kwenda Dar es Salaam  kwa hoja za msingi kwa manufaa na maendeleo ya Taifa 
7.   Tunaikumbusha serikali juu ya ahadi walizoahidi kuwafanyia wakazi wa kusini ambazo hazijatekelezwa na hazina muendelezo wowote ule kama ifuatavyo;
a)   Serikali iliahidi kujenga Tawi la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mkoani Mtwara.
b)  Serikali pia iliahidi kujenga Hospitali ya Rufaa katika mikoa ya Lindi na Mtwara.
c)   Kuzorota kwa utekelezaji wa mpango wa Mtwara Corridor hadi hivi leo.
Tunaomba Rais na wananchi wote kwa ujumla watuelewe kwamba, hatuna maana kwamba gesi yote ya Lindi na Mtwara itumike kwa wananchi wa Lindi na Mtwara tu, bali Kiwanda au Mitambo ya kufua umeme wa Gesi ijengwe Lindi na Mtwara na sio Dar es Salaam.

ENDAPO SERIKALI ITASHIKILIA MSIMAMO WAKE WA KUSAFIRISHA GESI ASILIA TOKA MNAZI BAY-MTWARA KWENDA DAR ES SALAAM BASI HATUA ZAIDI YA HII ITACHUKULIWA.

 TUUNGANE PAMOJA KUJENGE TAIFA LETU
Ahsanteni.


0 comments:

Post a Comment