Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Inspekta Jenerali Said Mwema
Habari za uhakika kutoka ndani ya Jeshi hilo zimedokeza kuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Inspekta Jenerali Said Mwema anatarajiwa kustaafu mwezi ujao na haijafahamika kama ataongezewa mkataba ama la.
Vyanzo mbalimbali vimedai kuwa japokuwa IGP Mwema
anasita kukubali kuongezewa muda, lakini Rais Jakaya Kikwete anaonelea
aongezewe muda ili wamalize pamoja uongozi wao mwaka 2015.
IGP Mwema ambaye alikuwa Ofisi ya Polisi wa
Kimataifa (Interpol) Jijini Nairobi, Kenya, aliteuliwa kushika wadhifa
wake huo mwaka 2006 na Rais Kikwete, kumrithi Omar Mahita ambaye
alistaafu.
Habari zinasema endapo IGP Mwema hatapewa mkataba
wa ama miaka miwili, basi ni dhahiri Rais Kikwete atakuwa na kibarua
kigumu cha kuanza mchakato wa kumtafuta mrithi wake.
IGP Mwema anachukuliwa kama mmoja wa viongozi wa
juu wa Jeshi hilo aliyelifanyia mapinduzi makubwa aliposhika madaraka
hayo, ikiwamo kuja na dhana ya ulinzi shirikishi ama Polisi Jamii.
Tayari mabadiliko hayo yameaanza kufanyika kwa
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni jijini Dar es Salaam, Charles
Kenyela kuhamishiwa makao makuu ya jeshi hilo.
Taarifa zaidi zimepasha kuwa nafasi nyingine ya
juu ambayo kuna dalili ya kuwepo kwa mabadiliko ni ya Mkurugenzi wa
Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), inayoshikiliwa na Robert Manumba.
Kwa mujibu wa taarifa za ndani ya jeshi hilo
aliyekuwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa (jina linahifadhiwa), amehamishiwa
makao makuu wakati tayari kuna taarifa za yeye kustaafu.
Hata hivyo, Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini,
Advera Senso alipotakia kueleza juu ya taarifa hizo za mabadiliko ndani
ya jeshi hilo, kutokana na muda wa kustaafu kwa maofisa hao kufika
alisema hizo ni taarifa za hisia.
“Hizo ni taarifa za hisia zako tu, lakini huwezi
kuniuliza swali la mwezi wa saba leo, tusubiri muda ukifika tuone
itakuaje,” alisema Senso.
Pia kuhusu taarifa za Kamanda wa Polisi Kinondoni,
Charles Kenyela kuhamishia makao makuu alisema; “Subirini nitatoa
taarifa kwani mbona kila mabadiliko yanayotokea ya makamanda huwa
ninatoa taarifa hivyo subirini”.
Habari zisizo rasmi zimelidokeza gazeti hili kuwa
huenda DCI Manumba akapumzishwa kutokana na hali yake ya kiafya
kuonekana kutorejea vizuri, licha ya kupatiwa matibabu nchini Afrika
Kusini.
MWANANCHI GAZETI
MWANANCHI GAZETI
0 comments:
Post a Comment