Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Tuesday 4 June 2013

JK aibua hofu mpya 2015

                                   

 
RASIMU ya Katiba mpya iliyotangazwa juzi na Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba nchini, Jaji Joseph Warioba, imeibua jambo zito linaloweza kusababisha kuahirishwa kwa uchaguzi mkuu wa 2015, Tanzania Daima Jumatano limebaini.
Uchambuzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa pendekezo la tume ya Jaji Warioba la kufanyia mabadiliko muundo wa muungano kutoka ule wa serikali mbili hadi serikali tatu kwa kuirejesha serikali ya Tanganyika, huenda likasababisha kuvurugika kwa ratiba ya uchaguzi mkuu ujao.
Kama rasimu hii itakubaliwa na wananchi katika kura ya maoni mapema mwakani, lazima uanzishwe mchakato mwingine wa kutafuta maoni ya wananchi wa Tanganyika kuhusu katiba ya jimbo lao jipya, hali inayoweza kusababisha kushindwa kufanyika kwa uchaguzi mkuu 2015.
Mtazamo wa Rais Jakaya Kikwete ni kukamilisha mchakato wa kuandika Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ifikapo Aprili 26, 2014, yaani mwaka mmoja tu kabla ya uchaguzi mkuu wa 2015, jambo linalofanya isiwepo nafasi ya kutosha ya kuanza na kukamilisha zoezi la kuandika katiba ya Tanganyika.
Maswali ya kujiuliza ni je, serikali imejiandaa kuanza mchakato mwingine wa kukusanya maoni ya Watanganyika kwa ajili ya katiba yao? Je, kutakuwa na fursa ya kutosha kufanya kazi hiyo kwa umakini, utulivu, na ufasaha ikizingatiwa kuwa uchaguzi mkuu utakuwa umebakiza mwaka mmoja tu kufanyika? Je, fedha za kuendesha zoezi hilo zitakuwepo?
Wadadisi wa mambo ya siasa wanabainisha kuwa kuna uwezekano mkubwa wa kutokea sintofahamu na songombingo ya kuvurugika kwa mifumo ya kitaasisi na kisheria inayotawala misingi ya mamlaka ya nchi, uongozi wake na utawala wa kitaasisi kwa kuwa tutahitaji mabadiliko ya mifumo ya kisheria inayounda taasisi nyingi za mamlaka ya serikali.
Hii inatokana na ukweli kwamba rasimu imependekeza mfumo wa serikali tatu, hivyo kutakuwapo na Serikali ya Shirikisho, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na serikali ya Tanganyika.
Mhadhiri SUA achambua
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe (SUA), Morogoro, Bakari Mohammed, anasema kuwa manadiliko hayo yakitokea maana yake ni kwamba mfumo wa serikali iliyokuwapo zamani lazima ubadilike kwa mujibu wa muundo wa Katiba mpya.
“Kwa kuwa muungano utakuwa wa “shirikisho” kwa maana kwamba ni jumuiya ya nchi zaidi ya moja zilizowekeana mkataba wa kuwa chini ya serikali na kiongozi mmoja ni dhahiri kwamba lazima mfumo wa msonge wa utawala na mamlaka ya serikali uliyopo sasa ubadilike,” anasema Bakari Mohammed.
Anasema mabadiliko hayo lazima yafuatiwe na kuufumua mfumo wa zamani unaotumika hata sasa na kuweka mfumo wa kisheria na kitaasisi utakaokubaliana na mfumo wa shirikisho.
“Na hili haliepukiki kwa kuwa ni jambo la lazima ili kuleta uwiano wa kitaasisi na kisheria katika uongozi na menejimenti ya serikali za nchi moja moja na ile ya shirikisho.”
Pia mhadhili huyo anasema mabadiliko ya muundo wa kisheria unaounda taasisi zenye mamalaka na madaraka lazima utahitaji muda wa kutosha kufanyika!
Kwa upande wa Zanzibar hakutakuwa na shida sana kwa kuwa tayari Wazanzibari walishakuwa na serikali yao kutokana na uwepo wa Katiba ya Zanzibar iliyofanyiwa upitizi na urekebu mwaka 2010.
Alisema tatizo linaloweza kuchukua muda wa utatuzi ni uwepo wa serikali ya Tanganyika ambayo kimsingi ilijipoteza yenyewe wakati wa mchakato wa kuunganisha nchi mbili. Tanganyika, kama nchi, haipo kwenye ramani ya siasa za muungano.
Hata hivyo, kwa mujibu wa kielelezo cha Katiba mpya inatakiwa irejeshwe ili ndio iingie kwenye shirikisho kama nchi ya pili mshirika katika kuunda Shirikisho la Jamhuri ya Tanzania.
Alisema kama dhana ya shirikisho ni ile inayofafanuliwa na maana ya shirikisho ni wazi kwamba hakuna shaka yoyote ya kutumia muda zaidi wa kuandaa mfumo wa sheria mama kwa nchi ya Tanganyika (Katiba ya Jamhuri ya Tanganyika) ambayo hadi sasa haipo!
“Na kwa jinsi hii ya kutokuwapo kwa Jamhuri ya Tanganyika na kukosekana kwa Katiba ya Jamhuri ya Tanganyika, ndivyo tunavyoweza kudhani kwamba, mchakato wa ukamilishaji wa uandishi wa Katiba mpya utaanzisha harakati nyingine za michakato ya kufumua miundo na mifumo ya kitaasisi na kisheria ili kuendana na utashi wa shirikisho,” alisema.
Msomi huyo alisema harakati za kuendesha michakato ya kuufumua mfumo wa Muungano wa sasa wa serikali mbili kuelekea serikali tatu chini ya shirikisho zinaweza kuchukua muda.
“Muda ni rasilimali muhimu sana kwenye michakato yoyote ile inayohitaji ukamilifu unaozingatia rasilimali hiyo. Na kutokana na muda ndivyo tunavyoweza kuangalia na kukokotoa gharama za kuendesha michakato yote inayokuja hapo baadaye.
“Inawezekana sana hakuna shaka juu ya matumizi ya rasilimali fedha zilizotengwa katika kuhakikisha kwamba mchakato wa kupatikana kwa Katiba mpya! Wasiwasi uliopo ni juu ya fedha na rasilimali nyingine katika kuwezesha uchakataji wa mabadiliko ya mifumo na au miundo ya kitaasisi na kisheria kuelekea shirikisho kwa mfumo wa serikali tatu unaopendekezwa,” alisema.
Alisema dhana inayojengwa hapa inaweza ikawiana sana na dhana ambayo imeshawahi kujengwa na Profesa Ibrahim Haruna Lipumba, Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) kwamba mchakato wa Katiba mpya unaweza ukamuongezea Rais Jakaya Kikwete muda wa urais.
Alisisitiza kuwa dhana hii inatokana na ukweli kwamba kwa vile haiwezekani kwa kazi inayokuja ya kufumua miundo na mifumo ya kitaasisi na kisheria ikafanyika kabla ya mwaka 2015.
“Hii ni kutokana na muda wa kazi na michakato yote, yaani uandishi wa Katiba ya Jamhuri ya Tanganyika, uandishi wa sheria mbalimbali zinazoanzisha taasisi mbalimbali zitakazokuwa na mamlaka na madaraka ya kikatiba kwa muundo wa shirikisho, na unadaaji wa mifumo ya kitaasisi kwa mujibu wa sheria zinazokubaliana na Katiba Mpya,” alisema.
Alisisitiza kuwa ukweli utabaki kwamba Tanganyika haina katiba na kwa vyovyote viwavyo haiwezekani kuwa na Serikali ya Shirikisho ambayo kuna nchi moja yenye katiba yake (Zanzibar) ilhali nchi nyingine haina katiba na hadi sasa haijulikani kwa kuwa haikuwapo.
Alisema kwa vile Tanganyika haipo kisheria,) lazima ifanye mambo yafuatayo.
Mosi kuandika katiba yake, pili iandae mifumo ya sheria zake kwa mujibu wa katiba yake, tatu iandae miundo yake ya kitaasisi kwa mujibu wa sheria zake zinazoafikiana na katiba yake na mwisho ifanye upitizi wa kimfumo unaoingiliana na mfumo uliopo kwenye nchi inayotaka kuingia nayo kwenye “shirikisho”, yaani Zanzibar.
“Hakika, kazi iliyoainishwa kwenye aya iliyotangulia inahitaji muda wa kutosha! Sidhani kama Tume ya Mabadiliko ya Katiba Tanzania imeliangalia suala hili kwa marefu, mapana na kina chake! Hata hivyo, inawezekana si kazi ya tume ya Jaji Warioba yenye jukumu la kuliangalia suala hili jipya linalokuja. Na sidhani kama Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa upande wake, imeliangalia jambo hili na au hata kupata muda wa kuliweka katika programu ya uandishi wa katiba hii (kifani inayotarajia kuingizwa kwenye hatua za mwisho katika kipindi kifupi kijacho),” alisema.
Uzoefu wa nchi jirani
Uzoefu wa nchi zingine zilizoandika Katiba mpya kama vile Kenya na Uganda unaonyesha kwamba unahitajika muda wa kutosha wa kutengeneza mfumo wa kisheria ili kuwezesha utekelezaji wa Katiba mpya.
Kwa mfano, Kenya walilazimika kurekebisha kalenda yao ya uchaguzi kwa kuamua kufanya uchaguzi mkuu wao Machi, 2013, badala ya Desemba, 2012, ili kuandaa mfumo wa kisheria na kitaasisi wa kuwezesha utekelezaji wa katiba yao mpya iliyokamilika mwaka 2010.
Mwanasheria Mkuu anena
Mwanasheria Mkuu wa Serikali Jaji Frederick Werema alipohojiwa na Tanzania Daima Jumatano kuhusu wasi wasi wa kuahirishwa kwa uchaguzi mkuu wa 2015 alisema kuwa serikali itafanya kila linalowezekana ili kuhakikisha uchaguzi huo unafanyika kama ilivyopangwa.
“Uchaguzi mkuu hauwezi kuahirishwa, serikali tutafanya kila linalowezekana kuandaa mazingira ya kuwezesha kufanyika kwa uchaguzi huo kwa wakati kama ilivyopangwa, kama ni Katiba ya Tanganyika na sheria zingine mbalimbali zitapatikana kwa wakati kabla ya 2015,” alisema Jaji Werema.
Katibu tume ya Katiba afafanua
Naye Katibu wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Assa Rashid alimwambia mwandishi wa habari hii kuwa siyo suala la Katiba ya Tanganyika pekee linalohitaji muda bali pia kuna mambo mengine mengi yanayohitajika muda kuyaweka sawa ili kuwezesha utekelezaji wa katiba mpya.
Alisema kuwa katika taarifa yake ya mwisho, tume itapendekeza kwa Rais Kikwete mambo mbalimbali ya kutekelezwa na utawala kwa lengo la kuwezesha kuanza kutumika kwa katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano na kwamba suala la upatikanaji wa katiba ya Tanganyika yawezekana likawemo katika mapendekezo yao.
“Kwa mujibu wa sheria ya mabadiliko ya katiba, tukimaliza kazi yetu tutawasilisha kwa Rais rasimu ya katiba mpya na taarifa ya tume ambayo itakuwa na maelezo na mapendekezo juu ya mambo mbalimbali yanayotakiwa kutekelezwa na serikali ili kuhakikisha katiba mpya inaanza kutumika, kwa hiyo inawezekana na hili la katiba ya Tanganyika likawemo katika taarifa yetu,” alifafanua Rashid.
Kwa upande wake Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Benson Bana, alisema hana wasiwasi kama uchaguzi mkuu 2015 unaweza kuahirishwa, kwani maoni ya wananchi wa Tanganyika yapo tayari ambayo yalipatikana wakati wa kukusanya maoni ya wananchi kwa ajili ya katiba ya Jamhuri ya Muungano, hivyo haitakuwa vigumu kupata katiba ya Tanganyika.
“Hapana, mimi sioni tatizo linaloweza kusababisha uchaguzi mkuu uahirishwe, kama ni suala la katiba ya Tanganyika tayari maoni ya wananchi yapo ambayo yalikusanywa wakati tume inakusanya maoni ya katiba ya Jamhuri ya Muungano, hivyo haitakuwa vigumu kupata katiba ya Tanganyika na ninafikiri ni vizuri tukapata katiba zote kwa wakati mmoja,” alisema Dk. Bana.
Hivi karibuni mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha Wananchi (CUF) Profesa Ibrahim Lipumba aliituhumu serikali ya Rais Kikwete kwamba ina mpango wa kujiongezea muda wa kukaa madarakani mpaka mwaka 2017.
Profesa Lipumba alidai kuwa mpango huo unatokana na kuwepo wasiwasi kuwa mchakato wa sasa wa kupata katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano hautaweza kukamilika ifikapo mwaka 2014, kama ilivyoahidiwa na Rais Kikwete mwenyewe.
Hata hivyo, hakuna ushahidi madhubuti unaoonyesha kama Rais Kikwete anafanya hila kutaka kuendelea kukaa madarakani baada ya kumaliza muda wake mwaka 2015, na kama itatokea akaendelea kukaa madarakani baada ya mwaka 2015 basi huo hautakuwa utashi wake ila ni hali halisi ya kisiasa.
Kibamba, Zitto wapongeza
MWENYEKITI wa Jukwaa la Katiba (JUKATA) Deus Kibamba ameipongeza Tume ya Jaji Wariona kwa kuandaa rasimu inayogusa mambo muhimu kwa maslahi ya taifa.
Pamoja na Kibamba, wengine walioipongeza tume hiyo ni wabunge, wanasiasa na wanaharakati ambao walizungumza na Tanzania Daima Jumatano kwenye viwanja vya Karimjee muda mfupi baada ya Jaji Mstaafu Joseph Warioba kuitangaza Rasimu ya Katiba mpya.
“Kwa kweli naipongeza tume; zipo kasoro kidogo za hapa na pale lakini kwa ujumla wake wamefanya kazi nzuri inayostahili pongezi,” alisema Kibamba.
Kuhusu hofu ya JUKATA kwamba muda wa kupata katiba mpya hautoshi alisema muda uliobaki ukitumika vema utatosha na kusisitiza kwamba ifikapo Aprili mwakani taifa litakuwa na katiba mpya iliyo bora.
Mbunge wa Kigoma Kaskazini Zitto Kabwe (CHADEMA) alisema rasimu ya katiba imeshindwa kugusa biashara ya kimataifa kwa kuiondoa nje ya masuala ya Muungano.
Kwa mujibu wa Zitto dosari hiyo inaweza kufanyiwa mabadiliko kwenye mabaraza na Bunge la Katiba huku akiipongeza tume ya jaji Warioba.
“Wazee wetu wamefanya kazi; wamejitahidi kadiri ya uwezo wao kuna maeneo hasa masuala ya Muungano wamefanya vizuri, kuwaondoa wabunge kuwa mawaziri kutaongeza uwajibikaji.
“…Suala la kimapinduzi ni lile la wananchi kuwaondoa wabunge wao ambao hawafanyi kazi vizuri kwa hivyo badala ya kusubiri miaka mitano wanaweza kumwondoa wakati wowote ni jambo jema,” alisema.
Kuhusu umri wa mgombe urais kuanzia miaka 40 Zitto ambaye ni Naibu Katibu Mkuu Tanzania Bara kwa CHADEMA, alisema anaheshimu uamuzi wa tume hiyo.
Kwa upande wake aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Dk. Asha-Rose Migiro alisema rasimu hiyo inatoa uwanja mpana kwa wananchi kushiriki kwenye uendeshaji wa nchi.
Kwa upande wake Waziri Mkuu wa zamani Dk. Salim Ahmed Salim alisema kutangazwa kwa rasimu hiyo kunaonyesha mwanga wa Katiba bora ya Tanzania inayozingatia Muungano.

0 comments:

Post a Comment