23Jumaadal Aakhir,1434 Hijiriyah/ May 03,2013 Miyladiyah
Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imesisitiza kuwa itaendeleza
utaratibu wa kuwafukuza wanafunzi wa vyuo vikuu ambao watakuwa na tabia
za utovu wa nidhamu na migomo isiyokuwa na lazima.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philip Mulugo.
Alisema
Serikali haina kigugumizi cha kuona ni kwa nini isiwafukuze wanafunzi
wa aina hiyo ambao wanakuwa ni kichocheo cha migogoro.
Alitoa kauli
hiyo wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Ubungo, John Mnyika
(Chadema), ambaye alitaka kujua mkakati wa Serikali kuwarudisha
wanafunzi wa vyuo vikuu ambao walifukuzwa masomo yao kutokana na
migogoro iliyoibuliwa vyuoni mwao.
Katika swali la msingi Mnyika
alitaka kujua hatua za Serikali katika kuwarudisha wanafunzi hao kutoka
vyuo vya Dodoma (Udom), Dar es Salaam na Chuo Kikuu Kishiriki cha
Sayansi (MUHAS).
Mbali na hilo, aliomba ripoti ya Tume ya Rais
iliyoundwa mwaka 2011 kwa ajili ya kuangalia migogoro hiyo kwa wanafunzi
ambayo imedumu kwa muda mrefu ili ipelekwe bungeni na kujadiliwa kabla
ya kumshauri Rais jambo la kufanya.
Naibu Waziri alisema katika
migogoro hiyo, kuna maeneo ambayo wanafunzi walisimamishwa masomo na
baadhi walirudishwa masomoni, lakini wengine bado hawajarudishwa.
“Mfano,
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, wanafunzi waliosimamishwa ni 99, lakini
78 walirudishwa na 21 hawajarudishwa, kwa Udom walisimamishwa 570 lakini
563 walirudishwa masomoni na 7 wamefukuzwa kabisa, kingine ni MUHAS
ambapo walisimamishwa wanafunzi 115 wengine wamerudi na wengine watarudi
Desemba mwaka huu wakati wanafunzi wawili wamefukuzwa kabisa,” alisema
Mulugo.
Kuhusu ripoti ya Rais, Mulugo alisema ilikuwa ni tume maalumu
kwa ajili ya kumsaidia Rais, hivyo siyo lazima ripoti yake kupelekwa
bungeni kama ambavyo wabunge wanataka.
Sikiliza Live
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment