Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Thursday, 29 November 2012

Palestina yatambuliwa na UN

Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa jana limeipandisha hadhi Palestina kwa wingi wa kura kuwa kama taifa lisilo mwanachama wa umoja huo. Rais wa Palestina Mahmoud Abbas ameshinda ombi lake aliloliwasilisha la kupewa hadhi hiyo. Abbas ameungwa mkono na nchi 138 wanachama wa baraza hilo lenye jumla ya wanachama 193. Nchi wanachama 41 wa baraza hilo hawakupiga kura huku nchi tisa zikipiga kura ya hapana, ikiwemo Marekani na Israeli. Ushindi huo wa Palestina umeonyesha kushindwa kidiplomasia kwa Marekani na Israeli ambazo ziliungwa mkono na mataifa machache kupinga hatua ya kuipandisha hadhi Palestina kutoka kuwa kama mtazamaji kwenye Umoja wa Mataifa na sasa kuwa kama taifa lisilo mwanachama wa umoja huo kama ilivyo kwa Vatican. Abbas amesema ushindi huo umepokewa kwa shangwe katika mji wa Ramallah, kwenye Ukingo wa Magharibi, ambapo watu wamejitokeza mitaani kushangilia. Hata hivyo, ofisi ya Waziri Mkuu wa Israeli, Benjamin Netanyahu imelaani vikali hatua hiyo kwa kile ilichokiita hotuba ya sumu kutoka kwa kiongozi huyo wa Palestina ambaye ameishutumu Israeli kutokana na propaganda za uongo. Netanyahu amesema hayo siyo matamshi ya kutolewa na mtu anayetaka amani na amesisitiza kwamba amani ya mashariki ya kati itafikiwa kwa mazungumzo ya ana kwa ana baina ya Palestina na Israeli.

0 comments:

Post a Comment