Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Tuesday 18 June 2013

Wakulima wamwaga dawa zenye kemikali vyanzo vya maji



Baadhi ya wakulima waliopo katika kata ya Malindi, wilaya ya Lushoto, wanadaiwa kumwaga dawa zenye kemikali za sumu katika vyanzo vya maji hali iliyozusha hofu kubwa kwa wakazi wa maeneo hayo kukumbwa na magonjwa hatari ikiwemo saratani.Hayo yamebainika baada ya uchunguzi uliofanywa na viongozi wa Baraza la Taifa la Hifadhi ya Mazingira (NEMC) kwa kushirikiana na Taasisi ya Hifadhi ya Mazingira ya Pamoja.
 Utafiti huo umebaini kwamba, baadhi ya wakulima wanaponyunyuzia dawa za kuulia wadudu waharibifu wa mazao katika bustani za mboga, vyombo wanavyowekea dawa hizo huvisafisha katika vyanzo hivyo vya maji.
 
 Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Taasisi ya Mazingira ya Pamoja, Stuart Hedi, wakulima wamekuwa wakitumia maji hayo kusafishia zana zao za kilimo kutokana na uelewa mdogo juu ya kanuni za afya na matumizi sahihi ya dawa hizo na athari zake kwa binadamu.
 
“Kila dawa ina kanuni za matumizi kama hutazifuata lazima kuna athari zitakazojitokeza na hii inatokana na kiwango cha uelewa kwa watumiaji sasa hawa wanahitaji kufuatiliwa kwa karibu na kuelimishwa kwa sababu jambo hili likiachwa athari zake ni kubwa kwani hata mboga wanazonyunyizia zina muda zinazotakiwa kukaa kabla ya kuvunwa” alisema Hedi.
 
Kwa upande wake, Afisa Mkuu Mwandamizi wa NEMC, Dk.Carlos Mbuta, alisema uchunguzi uliofanywa katika vijiji vya Lukozi na Mnadani vilivyopo katika kata ya Malindi, umeonyesha kuwa baadhi wakulima hawazingatii maelekezo ya maafisa ugani wakati wa kunyunyiza dawa hizo katika mazao yao, hivyo pia wanahatarisha maisha ya watumiaji wa mboga maeneo ya mjini ambao ndio wateja wao wakubwa.
 
“Athari hizi kwa hali hii inaweza zisitokee kwa watumiaji wa maji tu kwenye vyanzo hivi, lakini hata kwa walaji wa mboga zinazozalishwa hivyo ni vema wakulima wakaelimishwa ipasavyo namna ya kutumia dawa hizi bila kuleta athari kwa walaji” alisisitiza Dk. Mbuta.
 
Mmoja wa wakulima wanaojihusisha na kilimo cha nyanya, kabichi na vitunguu, Jumaa Mngazija, alisema hatua hiyo inatokana na baadhi ya wakulima kukataa kuheshimu sheria ndogo ndogo zilizotungwa na serikali za vijiji, ambapo  baadhi yao huendelea kumwaga kwa makusudi kemikali hizo.
 
Naye Afisa Ugani wa Kata ya Malindi, Kimomwe Halifa, alisema wakulima wamekuwa wakaidi licha ya kupewa elimu ya matumizi ya dawa hizo na kuwataka kuacha vitendo hivyo kwa sababu athari zake sio tu zitawakumba walaji wa mboga bali hata wao wenyewe na familia zao kutokana na matumizi ya maji hayo yanayomwagiwa kemikali zenye sumu.

0 comments:

Post a Comment