Rais Jakaya Kikwete akizungumza na vyombo vya habari siku za hivi karibuni
Rais Jakaya Kikwete anatarajiwa kuwasili mjini Dodoma, ambapo
pamoja na mambo mengine atakutana na Kamati ya Bunge ya Bajeti ikiwa
siku chache kabla ya kuwasilishwa kwa Bajeti Kuu ya Serikali
itakayoainisha Mapato na Matumizi yake kwa mwaka wa fedha 2013/14, Juni
13.
Kamati hiyo inayoongozwa na Mbunge wa Bariadi
Magharibi, Andrew Chenge imekuwa na vikao karibu kila siku, wakati
mwingine vikimalizika usiku ili ikijiweka sawa kabla ya
kuwasilishwa kwa Bajeti Kuu ya Serikali.
Habari zilizopatikana zinaeleza kuwa Rais Kikwete
akiwa mjini Dodoma atakutana na baraza lake la mawaziri na Kamati ya
Bajeti ili kupata picha ya mwelekeo wa bajeti, ambayo sehemu kubwa
imeelezwa kubanwa na upatikanaji wa fedha za kutosha kwa ajili ya
kuziwezesha wizara na taasisi zake kwa shughuli za kawaida na maendeleo.
Hata hivyo, habari zinadai kuwa ugumu uliopo ni
namna ya kupata fedha kwa asilimia 100 kwa ajili ya kutekeleza shughuli
mbalimbali za maendeleo na matumizi ya kawaida kwa wizara na Idara za
Serikali.
Chanzo chetu kilieleza kuwa pamoja na 'kukuna
kichwa' jinsi ya kupata fedha hizo, hata utekelezaji wa bajeti ya
2011/12 na 2012/13, ulikuwa mgumu kwa kuwa baadhi ya wizara na
taasisi zake zilipata nusu ya bajeti iliyopitishwa au asilimia 30 ya bajeti nzima.
Upatikanaji wa fedha hizo chini ya asilimia
unatarajiwa kwa wizara na taasisi zake huku ikielezwa kuwa ni kutokana
na kumegwa kwa asilimia za mafungu kulikosababishwa na kuongezeka kwa
matumizi ya Serikali zikiwemo dharura.
Chanzo kilipasha kuwa, wakati hali ikiwa hivyo,
hadi kufikia juzi kila Wizara ilishawasilisha taarifa zake mbele ya
kamati hiyo iliyokuwa ikikutana katika Ukumbi wa Pius Msekwa mjini
Dodoma, huku wizara nyingi mbali na kuwasilisha taarifa za mafungu yao
ya bajeti kwa mwaka 2013/14, zimeomba kuongezewa kasima kama kuna
uwezekano.
Itakumbukwa, wakati akiwasilisha bajeti ya mwaka
2012/13 Juni 14 mwaka jana, Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa alisema
kuwa bajeti hiyo imelenga kukabiliana na changamoto za uchumi ikiwa ni
pamoja na kuongeza fursa za kuuza, kushughulikia uhaba wa chakula nchini
na kupambana na mfumuko wa bei.
Alisema pia kuwa mpango wa Serikali ni kuendelea
kuimarisha ukusanyaji wa mapato, kusimamia matumizi, kushughulikia
ukosefu wa ajira hasa kwa vijana na kuwekeza katika miundombinu ya
nishati ya umeme hasa ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara hadi Dar es
Salaam.
Kingine alichokisema ni ujenzi wa barabara,
bandari na reli ya kati ili kupunguza gharama za kufanya biashara na
kuongeza tija katika uzalishaji; pamoja na kulipa madeni ya ndani na
nje.
0 comments:
Post a Comment