Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imelaani vikali mradi
mkubwa wa serikali ya Marekani wa kuwafanyia ujasusi watumiaji wa
Intaneti duniani. Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Sayyid
Abbas Araqchi akizungumza na waandishi habari Tehran Jumanne hii
amesema, ujasusi wa Marekani katika mitandao ya Intaneti 'si jambo
jipya' na kuongeza kuwa ujasusi huo unakiuka misingi ya demokrasia
ambayo Marekani inadai kuitetea.
Hivi karibuni gazeti la The Guardian la Uingereza
lilifichua namna Shirika la Usalama wa Taifa Marekani NSA linavyochukua
habari za kijasusi kutoka kwa mabilioni ya watumiaji wa Intaneti
duniani.
Kuhusiana na kadhia ya Syria, Araqchi amesema, Iran inaunga
mkono juhudi za Russia za kuandaa kongamano huko Geneva kwa lengo la
kuutatua mgogoro wa Syria kwa njia ya mazungumzo. Amesema kikao hicho
kitafanikiwa iwapo kitazishirikisha nchi zote ambazo zinaweza kuwa na
nafasi ya kusaidia utatuzi wa mgogoro wa Syria. Kuhusiana na uchaguzi
ujao wa rais wa Iran, Araqchi amesema, Wairani waishio katika nchi 96
duniani watapata fursa ya kupiga kura katika ofisi 128 za kibalozi za
Iran. Aidha ametoa wito kwa nchi zote hasa za Ulaya kulinda vituo vya
kupigia kura vya Iran na kutoruhusu makundi ya kigaidi kuvurga zoezi
hilo la uchaguzi.
0 comments:
Post a Comment