Wizara ya Mambo ya Ndani ya Iran imetangaza majina ya
watu 8 ambao wameidhinishwa kugombea kiti cha urais baada ya kuchunguzwa
na Baraza la Kulinda Katiba.
Walioidhinishwa kugombea kiti cha urais wa Jamhuri ya
Kiislamu ya Iran ni pamoja na mwakilishi mkuu wa Iran katika mazungumzo
ya nyuklia Saeed Jalili, spika wa zamani wa bunge Ghulam Ali Haddad
Adel, kamanda wa zamani wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu
Mohsen Rezai, mwakilishi wa zamani wa Iran katika mazungumzo ya nyuklia
Sheikh Hassan Rohani, makamu wa zamani wa rais Mohammad-Reza Aref,
waziri wa zamani wa mawasiliano Mohammad Gharzi, meya wa Tehran Mohammad
Bagehr Qalibaf na waziri wa zamani wa mambo ya nje Ali Akbar Velayati.
Rais wa zamani wa Iran Sheikh Hashemi Rafsanjani na mkuu
wa Ofisi ya Rais, Esfandiyar Rahim Mashaei hawakuidhinishwa kugombea
urais katika kipindi hiki.
Uchaguzi wa rais wa awamu ya 11 utafanyika Juni 14 na
mshindi wa uchaguzi huo atachukua nafasi ya Rais Mahmoud Ahmadinejad
anayemaliza muda wake na ambaye kwa mujibu wa katiba hawezi kugombea
mara hii baada ya kuhudumu kwa mihula miwili mfululizo.
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani Seyyed Solat Mortazavi
alitoa taarifa siku ya Jumamosi na kusema kampeni zitaanza rasmi baada
ya Baraza la Kulinda Katiba kutangaza orodha rasmi ya wagombea. Kampeni
zitamalizika masaa 24 kabla ya kuanza zoezi la uchaguzi.
0 comments:
Post a Comment