Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania
amekemea vikali vurugu zilizotokea jana mkoani Mtwara kusini mashariki
mwa nchi hiyo baada ya kusomwa bungeni kwa Bajeti ya Wizara ya Nishati
na Madini.
Akizungumza mjini Dodoma, Rais Kikwete
amesema wote waliohusika na vurugu hizo watasakwa na kuchukuliwa hatua
kali. Aliongeza kuwa rasilimali inayopatikana mahali popote pale nchini
inatakiwa kutumiwa na Watanzania wote. Akizungumza bungeni jana Waziri
wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo alisema mradi wa
kusafirisha gesi kutoka mkoani Mtwara kwenda Dar es Salaam, umeanza kwa
kasi na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda atakwenda huko wiki ijayo kuweka jiwe
la msingi. Tamko hili la Muhongo ndilo lililoibua vurugu kubwa Mtwara.
Aidha jambo lingine linalosemekana limesababisha ghasia hizo ni hatua ya
Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kutokurusha moja kwa moja
matangazo ya Bunge hivyo kuwakosesha wananchi fursa ya kusikiliza bajeti
hiyo. Baadhi ya duru zinasema mtu mmoja amefariki dunia na wengine
kadhaa kujeruhiwa kutokana na vurugu hizo. Milio ya risasi za moto na
mabomu ya machozi vilisikika katika maeneo kadhaa ya Mtwara ambako hali
ilikuwa mbaya kutokana na kuzuka mapambano kati ya polisi na vijana
waliokuwa na hasira.
0 comments:
Post a Comment