Umoja wa Mataifa umetangaza kuwa kundi la waasi wa Lord's Resistance
Army LRA la nchini Uganda limetekeleza jinai kubwa za kuua maelfu ya
watu katika eneo la Afrika Mashariki na ya Kati. Taarifa ya Umoja wa
Mataifa imeeleza kuwa, kundi hilo linaloongozwa na Joseph Kony ambaye
anasakwa na Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC, limewaua zaidi ya watu
laki moja katika eneo hilo katika kipindi cha miaka 25 iliyopita. Ban Ki
moon, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amesema kuwa, kundi la LRA
linatuhumiwa kuwakamata mateka watoto baina ya elfu sitini hadi laki
moja na kusababisha pia watu wengine wasiopungua milioni mbili na nusu
kuwa wakimbizi. Wakati huohuo, Navi Pillay Kamishna Mkuu wa Haki za
Binadamu wa Umoja wa Mataifa amesema kuwa, hivi karibuni itatolewa
ripoti ya jinai zilizofanywa na kundi la LRA tokea mwaka 1988. Inafaa
kuashiria hapa kuwa, kundi la LRA lilianzisha uasi kaskazini mwa Uganda
mwaka 1988, kisha likaelekea na kujizatiti katika maeneo ya mashariki na
kaskazini mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Jamhuri ya Afrika ya
Kati na Sudan Kusini mwaka 2005.
Sikiliza Live
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment