“Harakati za Fat – h na Hamas
zimeshaipita awamu ya uhasama, na harakati ya Hamas inakubaliana na
kuundwa serikali itakayoongozwa na Mahmoud Abbas”. Hayo ni matamshi
yaliyotolewa na Musa Abu Marzouq, Naibu Mkuu wa Idara ya Kisiasa ya
Harakati ya Muqawama wa Kiislamu ya Palestina HAMAS alipozungumza na
waandishi wa habari juzi Jumanne kuelezea uwezekano wa kuundwa serikali
mpya ya maridhiano ya kitaifa ya Palestina. Katika mazungumzo hayo na
waandishi wa habari Abu Marzouq alitoa ufafanuzi wa vikao vya kutafuta
mwafaka wa maridhiano ya kitaifa baina ya Wapalestina vilivyofanyika
hivi karibuni mjini Cairo Misri, lengo hasa likiwa ni kuondoa mpasuko wa
ndani baina ya harakati na taasisi za Kipalestina za Gaza na Ramallah
na kueleza kwamba Hamas inakaribisha kuundwa kwa serikali ijayo
itakayoongozwa na Mahmoud Abbas, Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina
ambayo itaandaa mazingira ya kufanyika uchaguzi huko Palestina.
Musa Abu Marzouq alizungumzia pia mpango
wa John Kerry, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani wa ubadilishanaji
ardhi kwa suluhu kati ya Wapalestina na utawala wa Kizayuni na kuundwa
dola la Kiyahudi katika ardhi zinazokaliwa kwa mabavu za Palestina na
kusisitiza kwamba lengo la mpango huo ni kuzihodhi kikamilifu ardhi zote
za Palestina.
Kwa mtazamo wa viongozi wa Hamas ili
kuweza kumaliza hitilafu za ndani, Mahmoud Abbas anapaswa kuyatambua
rasmi makundi yote ya Palestina yanayotaka kushiriki kwenye uchaguzi wa
Baitul Muqaddas na kuandaa mazingira ya kufanyika uchaguzi huru
utakaoshirikisha makundi yote ya Palestina huko Ufukwe wa Magharibi wa
Mto Jordan.
Safari ya hivi karibuni ya Mahmoud Abbas
katika Ukanda wa Gaza iliyofanywa kwa lengo la kuleta umoja kati ya
eneo hilo na lile la Ufukwe wa Magharibi ilipokewa kwa mikono miwili na
viongozi wa Hamas; na hivi sasa Gaza inasubiri kwa hamu hatua muhimu
inayopaswa kuchukuliwa na Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina ya
kuunda serikali ya umoja wa kitaifa ili kufungua njia ya kufanyika
chaguzi mbili muhimu za bunge la Palestina na Rais wa Mamlaka ya Ndani.
Na hasa kwa kuzingatia kwamba hivi karibuni Mahmoud Abbas mwenyewe
alitamka bayana kuwa siasa za utawala wa Kizayuni wa Israel ni za kutaka
kujitanua na kwamba ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kizayuni ndicho
kizuizi kikuu cha kuanza kufanya tena mazungumzo na utawala huo
ghasibu. Hii inamaanisha pia kwamba baada ya kupita miaka 20 ya
mazungumzo na Israel viongozi wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina
wameshafika mwisho wa njia na wanahisi kuwa kuendelea na safari hiyo
kutawaelekeza kusikojulikana. Mahmoud Abbas amesisitiza kwamba viongozi
wa Palestina wanafungamana na suluhu kamili na ya kiadilifu
itakayowahakikishia kuwa wanafikia lengo lao la kuunda nchi huru ya
Palestina katika mipaka ya mwaka 1967. Kesho Ijumaa, Abbas anatazamiwa
kukutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani
John Kerry huko Ramallah. Itakumbukwa kuwa tangu tarehe 23 Machi mwaka
huu Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani ameanzisha harakati za kuyafufua
mazungumzo yaliyokufa kati ya Mamlaka ya Ndani ya Palestina na utawala
wa Kizayuni wa Israel, hata hivyo harakati hizo za kidiplomasia za White
House hadi sasa zimegonga ukuta kutokana na siasa za kushupalia vita na
za kujitanua za utawala haramu wa Israel…/
0 comments:
Post a Comment