Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Thursday 16 May 2013

Hali tete Mtwara

                         

HALI ya mambo huenda ikavurugika tena mkoani Mtwara baada ya kuwepo kwa taarifa za maandalizi ya mgomo na maandamano ya kudai kunufaika na gesi.
Mwishoni mwa mwaka jana wananchi wa Mtwara walifanya maandamano kupinga ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam uliopangwa kutekelezwa na serikali.
Februari mwaka huu wananchi hao waliamua kufanya maandamano mengine yaliyoambatana na vurugu ikiwemo kuchoma nyumba za viongozi wa CCM.
Baada ya kutokea matukio hayo, viongozi mbalimbali wa serikali, akiwemo Waziri Mkuu, walikwenda kuzungumza na wananchi hao jinsi ambavyo wangelinufaika na gesi hiyo.
Miongoni mwa ahadi walizopewa ni kuboreshwa kwa bandari ya Mtwara, kujengwa kwa kiwanda cha saruji na uwanja wa ndege wa kisasa ambavyo vitachangia kukua kwa uchumi wa mkoa huo.
Tanzania Daima limedokezwa kuwa baadhi ya watu wamesambaza vipeperushi mitaani kuwahamasisha wananchi kujiandaa kusikiliza na kuangalia hotuba ya Wizara ya Nishati na Madini.
Kwa mujibu wa baadhi ya wananchi, vipeperushi hivyo vinawataka wasifanye shughuli yoyote siku bajeti hiyo itakaposomwa ili wajue hatima ya gesi iliyoko mkoani mwao.
“Tuliambiwa leo bajeti ya Nishati na Madini itasomwa lakini baadaye tunaambiwa itasomwa wiki ijayo…hapa watu wamejipanga kuifuatilia,” alisema Nchiman Joseph.
Moja ya vipeperushi kilisomeka: “Zinduka kusini, wananchi kwa pamoja. JK ameamua kutumia nguvu kwenye suala la gesi.
“Kwa pamoja Mei 17, 2013 saa tano asubuhi tukusanyike kwenye vituo vya runinga ili kusikiliza bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini; tutambue vema sakata la gesi, sambamba na hilo tusitishe huduma zote za jamii ikiwemo bodaboda, teksi, bajaji na magari ya abiria-zinduka Mtanzania!”
Tanzania Daima imedokezwa kuwa Kamanda wa Polisi mkoa wa Mtwara, Linus Sinzumwa, ameonekana katika kituo cha redio kiitwacho Pride FM kuwatahadharisha wananchi kuhusu vipeperushi hivyo.
Kamanda huyo aliwaambia wananchi wasihofu juu ya usalama wao kwa kuwa polisi imejipanga kuhakikisha vurugu zilizotokea huko nyuma hazitokei tena.
Tanzania Daima iliwasiliana na Kamanda Sinzumwa ambaye alikiri kuna taarifa za vipeperushi hivyo na kuwataka wananchi wavipuuzie.
“Ni kweli vipeperushi vipo ila hali ni shwari…, nyie mnataka kukuza tu, nimeshatoa tahadhari na tutafanya udhibiti mkubwa sana,” alisema.
Nyumba za kulala wageni
Chanzo chetu cha taarifa kimedokeza kuwa nyumba ya kulala wageni zilikuwa na wegeni wengi ambao wengine wakisadikiwa ni askari kutoka makao makuu ya jeshi la polisi.
Mmoja wa wananchi alizungumza na gazeti hili kwa simu alisema: “sisi wananchi wa Mtwara tumekuwa gizani kwa kipindi kirefu bila kujua lengo la serikali katika suala la gesi ambayo itachimbwa huku tumekubaliana na masuala ambayo tuliyataka yatolewe ufafanuzi ambapo serikali haikufanya hivyo.”
Aliongeza kuwa wananchi wanataka kuona mambo waliyokubaliana na serikali katika mikutano mbalimbali yanatekelezwa kwa kuwekwa katika bajeti hiyo.
“Sisi hatuna ugomvi na serikali; tunachotaka ni kuona utekelezaji wa masuala tuliyokubaliana yanakuwepo katika bajeti ambayo kwetu yatatuwezesha kuendelea kiuchumi na sio kuonekana wazalishaji lakini wananufaika wengine,” alisema Mpendela.
Baadhi ya wananchi hao walilalamika kuwa suala la gesi linapelekwa kisiasa huku wananchi wakiwa njia panda bila kujua ni maslahi gani watakayonufaika nayo.
Shura ya Maimamu
Viongozi wa Shura ya Maimamu ni miongoni watu waliofanya mazungumzo na kamanda wa polisi mkoa wa Mtwara juu ya tisho la vurugu.
“Sisi tumefanya vikao sio leo tangu juzi, kamanda wa polisi alituita ingawa yeye bado ni mgeni alitaka tujadili suala la amani ya mji wa Mtwara na dhana ya utii wa sheria bila shuruti katika kikao hicho tuliunda kamati ya watu 10, Wakristo watano na Waislamu watano.
“Leo alituita ili tujadili ni nani anahusika na vipeperushi hivi. Kwa hiyo tumetoa tamko kuwa kesho wananchi waendelee na shughuli zao kwani siku ya kesho sio ya kujadili Bajeti ya Nishati na Madini, tumemkabidhi kamanda wa polisi wa mkoa aende kwenye vyombo vya habari kuisoma ili awaarifu wananchi,” alisema mmoja wa viongozi wa taasisi hiyo.
Kiongozi huyo alitaka elimu iendelee kutolewa kwa wananchi ili mtoaji wa vipeperushi hivyo ajulikane.
“Hatutaki vurugu zitokee hii leo,…. maana wengine wanaweza wakaleta dhana ya udini ikaonekana Waislamu wametengeneza au Wakristo wanatumia mwanya huo kuharibu Ijumaa.
 

0 comments:

Post a Comment