Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Sunday 21 April 2013

Waislamu wazuiwa kujenga msikiti Ufaransa

                             12Jumaadal Aakhir,1434 Hijiriyah/ April 22,2013 Miyladiyah
 Waislamu wa mji wa Montrouge nchini Ufaransa wamepanga kufanya maandamano makubwa ya kulalamikia hatua ya manispaa ya mji huo ya kupinga kujengwa msikiti mjini humo. Kituo cha habari ya Echo-Montrouge kimewataka Waislamu wa mji wa Montrouge wa kusini mwa mji mkuu wa Ufaransa, Paris, kujitokeza kwa wingi kwenye maandamano hayo ili kulalamikia hatua ya manispaa ya mji huo ya kuzuia kujengwa kituo pekee cha ibada kwa Waislamu mjini humo. Maandamano hayo yamepangwa kufanyika wiki ijayo yaani Aprili 27, na mkuu wa Jamii ya Waislamu wa Ufaransa, Nabil an Nasri, na mkuu wa jamii ya kupambana na chuki dhidi ya Uislamu, Sami Dabbah, watahutubia waandamanaji na kusisitiza juu ya haki ya Waislamu wa mji huo ya kuwa na msikiti. Jumuiya ya Kudumisha Udugu ya mji wa Montrouge ndiyo iliyoitisha maandamano hayo na imewataka wananchi wote wa Ufaransa kushiriki kwenye maandamano hayo. Ujenzi wa msikiti katika mji wa Montrouge huko Ufaransa ulianza miaka minne iliyopita lakini miezi miwili tu tangu kuanza ujenzi huo, manispaa ya mji huo iliingilia kati na kuzuia kuendelea kujengwa sehemu hiyo ya ibada kwa Waislamu. Waislamu wa Ufaransa walipigania sana haki yao hiyo na mwaka huu wa 2013 wamepewa tena kibali ya kuendelea kujenga msikiti huo lakini hivi sasa pia manispaa ya mji wa Montrouge imeingilia tena kati na kuzuia ujenzi huo kwa madai kuwa Waislamu mjini humo ni wachache hivyo hawana haki ya kuwa na msikiti.

0 comments:

Post a Comment