Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Tuesday 16 April 2013

Vijana wa Veta kufyatua matofali ya NHC






Mkakati wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) wa ujenzi wa nyumba 15,000; zikiwamo 5,000 za gharama nafuu katika maeneo mbalimbali nchini, umepamba moto, baada ya NHC na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (Veta), kutiliana saini makubaliano ya utoaji wa mafunzo kwa vijana 35 ya kutengeneza matofali kwa ajili ya mradi huo.
 
Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Nehemia Mchechu, alisema jana kuwa vijana hao; wakiwamo wanaume 32 na wanawake watatu, ni kati ya 60 waliotafutwa na Veta kutoka mikoa 16 ya Tanzania Bara, ambayo kwa sasa ina ujenzi wa nyumba za gharama nafuu.
 
Mchechu alisema hayo katika hafla ya utiaji saini makubaliano na uzinduzi wa mafunzo hayo kwa vijana hao, iliyofanyika Veta, jijini Dar es Salaam jana.
 
Alisema Veta kwa kushirikiana na NHC, iliwachuja vijana 60 kupitia usaili makini uliofanyika wiki iliyopita na kuwabakisha 35, ambao watatafundishwa kwa wiki mbili kuanzia jana, kutengeneza tofali kwa kutumia teknolojia mpya ya mashine za “Hydraform”. 
 
Mchechu alisema anatarajia ushirikiano uliowezesha kuwapata vijana hao, utakuwa na manufaa makubwa kwa kuwa utawezesha ujenzi wa nyumba 1,054 ndani ya mwaka mmoja na kwamba matofali 5,270,000 yenye gharama ya Sh. bilioni 3.162 yatatengenezwa na vijana hao.
 
Aliwahakikishia vijana hao kuwa baada ya kumaliza mafunzo yao watawachukua kwa mkataba wa mwaka mmoja na kuwapeleka katika maeneo ambayo watashiriki kufyatua matofali na kujenga nyumba za gharama nafuu.
 
Awali, Mkurugenzi wa Uendelezaji Milki wa NHC, Benedict Kilimba, alisema baada ya kupata mafunzo hayo, vijana hao watasambazwa katika mikoa mbalimbali, ikiwamo Dar es Salaam, Morogoro, Dodoma, Tanga, Singida, Manyara, Lindi, Kigoma, Ruvuma na Katavi, kufanya kazi hiyo.
 
Mchechu alisema mashine 15 za aina hiyo zimenunuliwa na kwamba kila moja ina uwezo wa kufyatua tofali 2,000 kwa siku.
 
Awali, Mkurugenzi Mkuu wa Veta, Zebadiah Moshi, alisema tatizo la ajira kwa vijana limekuwa kilio kikubwa nchini, hivyo hatua hiyo itasaidia kwa kiwango kikubwa.
 
Hata hivyo, alisema kulingana na utafiti uliofanyika kwa miaka mitatu, kati ya vijana wanaomaliza vyuo, asilimia 66 hupata ajira na kwamba, wanapenda iongezeke kufikia asilimia 95 katika kipindi cha miaka mitano.



0 comments:

Post a Comment