Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Tuesday 9 April 2013

Uhuru aapishwa kuwa rais wa nne wa Kenya

 Uhuru Kenyatta ameapishwa leo kuwa Rais wa Nne wa Kenya katika sherehe iliyohudhuriwa na makumi ya maelfu ya wafuasi wake waliojawa na furaha pamoja na viongozi zaidi ya 20 kutoka nchi kadhaa za Afrika. Katika hotuba yake baada ya kula kiapo, Kenyatta ambaye ni mwana wa Rais wa Kwanza wa Kenya hayati Mzee Jomo Kenyatta amesema atawahudumia Wakenya wote pasina kuwepo ubaguzi. Ametoa wito kwa Wakenya wote kudumisha umoja na amani. Rais Kenyatta amesema katika siku 100 za kwanza za utawala wake ataondoa malipo ya huduma za uzazi  na halikadhalika wananchi watapata matibabu katika zahanati za serikali pasina kutoa malipo. Vile vile amesema shilingi bilioni sita ambazo zilikuwa zimetengwa kwa ajili ya duru ya pili ya uchaguzi zitatumika kuanzisha mfuko mpya wa vijana na wanawake kote nchini Kenya. Amesema, serikali yake itabuni nafasi za kazi hasa kwa ajili ya vijana. Kuhusua masuala ya kimataifa amesema Kenya itaheshimu majukumu yake ya kimataifa kwa msingi wa kuheshimiana. Amesema hakuna nchi yoyote inayopaswa kuhodhi au kudhibiti taasisi za kimataifa au kufasiri mikataba ya kimataifa. Amesema kila nchi ina haki ya kuwa na mtazamo wake ambao unapaswa kuheshimiwa na mataifa mengine.

0 comments:

Post a Comment