Tume ya Kuchunguza Matokeo Mabaya ya Kidato cha Nne ya mwaka 2012 iliyoundwa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda imemaliza kukusanya maoni ya awamu ya kwanza katika mikoa ya Dodoma, Uguja na Pemba na imeanza awamu ya pili.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Katibu wa Tume
hiyo Edwin Mgendela, alisema kazi hiyo inaendelea vizuri na wananchi
wamekuwa wakijitokeza kwa wingi kutoa mawazo yao na kwamba awamu ya
kwanza kwenye mji wa Dodoma, Pemba pamoja na Unguja lilimalizika Ijumaa
iliyopita.
Alisema katika awamu ya kwanza mkoani Dodoma, Tume ilitembelea
Ofisi ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) na baadhi ya
halmashauri za mkoa huo na kutembelea shule ilizoelekezwa na katika
awamu ya pili iliyoanza jana wajumbe watatembelea vyuo vinavyoandaa
walimu kikiwemo Chuo cha Elimu cha Capital, Chuo cha Elimu Mpwapwa na
Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom).
“Kimsingi ziara hiyo inalenga kuangalia na kupata taarifa za namna
walimu wanavyoandaliwa, ikiwa ni pamoja na changamoto wanazokumbana nazo
katika kuwapika walimu hao pamoja na kupata mtazamo wao,” alisema
Mgendela.
Alisema katika awamu ya pili, wajumbe pia watakwenda Dodoma ili
kuonana na wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii, inayoongozwa
na Margareth Sitta ili na wao waweze kutoa maoni yao Aprili 11.
Aidha wajumbe wengine watakwenda Zanzibar ili waweze kuonana na
Kamati kama hiyo ya Baraza la Wawakilishi, ili na wao watoe maoni yao.
Mgendela alisema kuwa wajumbe wa Tume hiyo kwa siku ya jana,
walitarajiwa kuonana na taasisi mbalimbali zinazomiliki shule ili na wao
watoe maoni yao.
0 comments:
Post a Comment