Powered by Blogger.

Sikiliza Live

Saturday 13 April 2013

Lugora adai baadhi ya mawaziri ni wauza unga

MBUNGE wa Mwibara, Kangi Ligora (CCM) amewalipua mawaziri  akidai kuwa baadhi yao ni wauzaji wakubwa wa dawa za kulevya na wala rushwa.
Bila kumung'unya maneno, mbunge huyo alisema kuwa tatizo hilo ni kikwazo kwa maendeleo ya uchumi wa taifa.
Lugora alitoa kauli hiyo jana wakati akichangia mjadala wa hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2013/2014.
Huku akisikilizwa kwa makini na mawaziri na wabunge wengi, Lugora alisema kuwa suala la rushwa na dawa za kulevya ni maadui wakubwa wa uchumi, lakini hotuba ya Waziri Mkuu haioneshi mikakati ya kupambana na maadui hao.
“Nimesoma gazeti siku moja nikashtuka kusikia kamishna wa kupambana na dawa za kulevya anasema kuwa anawajua wauza unga, lakini wanashindwa kuwakamata kutokana na mbinu zao. Serikali inamwachia kwanini isimwajibishe?” alisema.
Aliongeza kuwa serikali inawajua wauzaji wakubwa wa dawa za kulevya, lakini inashindwa kuwakamata na kuwafikisha mahakamani kutokana na rushwa.
Lugora ambaye ni mmoja wa wabunge wa CCM wanaotoa hoja nzito za kuikosoa serikali, alisema kwa bahati mbaya kila utafiti unapofanyika waathirika wakubwa wa rushwa ni polisi.
Alishauri kuwa ili polisi wa kima cha chini waache kupokea rushwa, waongezewe mishahara. Pia aliiponda hotuba ya Waziri Mkuu kwamba haina mikakati ya kuondokana na hali hiyo badala yake imekuja na lugha nzuri ya kuwalaghai wabunge na wananchi.
Aliishangaa ofisi ya Waziri Mkuu kutenga sh bilioni moja kwa ajili ya mazishi ya viongozi wakati asipokufa kiongozi yeyote kwa kipindi hicho fedha hizo hazirejeshwi wala Bunge halijulishwi zimetumikaje.
Hata hivyo kauli ya Lugora kudai kuwa baadhi ya mawaziri ni wauza dawa za kulevya, ilionekana kuichefua serikali ambapo Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Uwezeshaji na Uwezeshaji), Dk. Mary Nagu alisimama na kuomba mwongozo wa spika akitaka mbunge huyo awataje kwa majina mawaziri hao au afute kauli yake.
Spika Makinda alimtaka Lugora afute kauli au awataje kwa majina kama alivyomtaka Waziri Nagu, lakini alishikilia msimamo wake akisema waziri alimwelewa vibaya.
 

0 comments:

Post a Comment