11Jumaadal Aakhir,1434 Hijiriyah/ April 21,2013 Miyladiyah
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali
Mohamed Shein amezitaka mamlaka za mikoa na serikali za mitaa
kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kudhibiti wimbi la wizi wa
mazao na mifugo lililoshika kasi Zanzibar hivi sasa.
Alisema suala hilo lazima lishughulikiwe vizuri na kwa umakini mkubwa
kwa sababu hatua iliyofikiwa sasa na vitendo vya baadhi ya wezi kukata
sehemu za viungo vya mifugo kama ng’ombe na kuwaacha wazima sio tu kuwa
ni ukatili bali pia haviwezi kufikiriwa kufanywa Zanzibar.
Dk. Shein alitoa wito huo wakati akihitimisha majadiliano ya mkutano
wa tathmini ya taarifa ya utekelezaji mpango kazi wa Ofisi ya Rais na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Idara ya Uratibu Mamlaka za Mikoa na
Serikali za Mitaa uliofanyika jana Ikulu.
“Ni vitendo vibaya na vya kikatili kukata baadhi ya viungo vya mnyama
bila kuchinjwa huku ukimwacha akihangaika kwa maumivu. Lazima tuwe
makini na hatua za kuchukua kwa kuwa wanaofanya vitendo hivi si watu wa
kawaida,” alisema.
Alisema hofu yake ni kuwa nyama hiyo huishia kuuzwa kwa matumizi
mbalimbali ya wananchi kitendo ambacho kinaingilia hata imani ya dini.
Sambamba na agizo hilo, Dk. Shein aliwakumbusha viongozi na watendaji
wa mamlaka hizo kuelewa kuwa ndizo zilizo karibu na jamii hivyo kila
wakati wawe tayari kupokea na kutafuta njia za kukabiliana na
changamoto.
“Huko mliko ndiko kwenye wananchi… sisi wote humu (kikaoni) tunaishi
katika maeneo ya mamlaka zenu, hivyo hoja zitakuja, malalamiko yatakuja
na hata pongezi wakati mwingine wananchi watakuja nazo, zote tuzipokee,”
alisema.
Sikiliza Live
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment